30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Watendaji waDART wafikishwa mahakamani

asteriaNA KULWA MZEE, DAR ES SALAAM

OFISA Mtendaji Mkuu wa DART, Asteria Mlambo, Mkurugenzi wa Fedha na Utawala, Evadius Katale na Mwanasheria Mkuu, Francis Kudesha, wamefikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuisababishia Serikali hasara ya Sh milioni 83.

Washtakiwa hao walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam jana wakitokea kazini na kusomewa mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi, Respicius Mwijage.

Wakili wa Serikali, Jacline Nyantori alidai mahakamani kwamba washtakiwa katika kesi hiyo ni Mlambo, Katale, Kudesha na mshtakiwa wanne Yuda Mwakatobe.

Alidai mshtakiwa wa kwanza hadi watatu wanadaiwa kati ya Septemba mosi na Oktoba 31 mwaka 2013, wakiwa katika nyadhifa zao walishindwa kutimiza majukumu yao kwa weledi na kusababisha hasara ya Sh. 83,564,367.

Nyantori alidai shtaka la pili linamkabili Mwakatobe, ambaye anadaiwa Juni 29, 2005 katika ofisi za kodi Mkoa wa Ilala, alitoa taarifa za fedha za uongo za Kampuni yake ya Yukan Business Ltd za mwaka 2004 na kusababisha afanyiwe makadirio ya chini ya kodi.

Shtaka la tatu linamkabili tena Mwakatobe, anayedaiwa kuwa Mei 25, 2006 aliwasilisha taarifa za hesabu za uongo za kampuni hiyo za mwaka 2005 na kusababisha akadiriwe kiasi cha chini cha kodi.

Washtakiwa wote walikana mashtaka na Wakili Nyantori alidai upelelezi haujakamilika na hawakupinga dhamana isipokuwa masharti yazingatie matakwa ya kisheria.

Hakimu Mwijage alisema mshtakiwa wa kwanza hadi watatu watadhaminiwa na mdhamini mmoja, atakayesaini dhamana ya maandishi ya Sh. milioni 15, awe na barua kutoka ofisi yoyote ya Serikali ama taasisi inayotambulika au kampuni iliyosajiliwa.

Pia washtakiwa wenyewe wanatakiwa kuwasilisha mahakamani hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya Sh milioni 14.

Hata hivyo, Hakimu Mwijage alisema sharti la kuwasilisha hati hata kama litakuwa halijakamilika, haliwezi kuzuia washtakiwa kupata dhamana, wanaweza kutimiza sharti hilo kwa muda utakaopangwa na mahakama.

Kwa upande wa mshtakiwa Mwakatobe, Hakimu Mwijage alisema atadhaminiwa na mdhamini mmoja, atasaini dhamana ya maandishi ya Sh milioni tano na awe na barua ya utambulisho kutoka ofisi za Serikali, taasisi inayotambulika ama kampuni iliyosajiliwa.

Washtakiwa wote walitimiza masharti ya dhamana isipokuwa Mwakatobe na kesi iliahirishwa hadi Machi 9, mwaka huu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles