AKURE, Nigeria
WATU wasiojulikana wameendelea kuwashikilia wanasoka wawili wa klabu za Eyinmba FC na Abia Comet na ujumbe wao ni kwamba wapewe Naira milioni 20 (zaidi ya Sh mil. 120 za Tanzania) ndipo wawaachie.
Wachezaji waliotekwa ni Dayo Ojo wa Enyimba FC ya Ligi Kuu, wakati mwenzake ni Benjamin Iluyomade anayeichezea Abia Comet inayoshiriki Ligi Daraja la Pili.
Aidha, tukio la kutekwa kwa nyota hao lilitokea jioni ya Jumapili ya mwishoni mwa wiki iliyopita katika moja ya mitaa ya Jimbo la Ondo.
Taarifa ya watekaji kutaka kiasi hicho cha fedha imetolewa na mmoja kati ya ndugu wa wachezaji hao, ambaye hata hivyo alikataa jina lake kuwekwa hadhrani.
Kile kilichoelezwa na mwanafamilia huyo ni kwamba watekaji walianza kwa kuhitaji Naira milioni 100, kabla ya kubembelezwa na kukubali kupokea hicho kilichotangazwa.