30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Wateja wa kuku waadimika Kisutu

JOHN KIMWERI Na AVELINE KITOMARY-DAR ES SALAAM

WAFANYABIASHARA wa kuku katika Soko la Kisutu jijini hapa wamelalamikia uhaba wa wateja na hivyo kusababisha biashara kuwa ngumu huku wakidai kuwa kiwango cha ushuru kiko juu.

Akizungumza na MTANZANIA jana, mmoja wa wafanyabiashara hao, Ramadhani Abeid alisema kuku ni wengi, lakini wateja hakuna.

Akitaja bei za kitoweo hicho, alisema kuku wa kienyeji anauzwa kati ya Sh 15,000 hadi 17,000 na kuku wa kisasa anauzwa Sh 10,000.

“Kuku ni wengi lakini wateja hakuna, kwa sasa kuku wa kienyeji ni Sh 15,000 hadi 17,000 na kuku wa kisasa ni Sh 10,000,” alisema Abeid.

Aidha alisema miongoni mwa sababu zinazosababisha ugumu wa biashara hiyo ni kuwa wanafunzi wengi wameanza kurudi shule pamoja na watu wengi kusafiri nje ya Dar es Salaam kutokana na sikukuu za Krismasi na Mwaka Mpya.

Mfanyabiashara mwingine, Mohamedi Ndete, alisema changamoto kubwa ipo kwa wafugaji kwakuwa kipindi hiki hawapati faida kutokana na ugumu huo wa biashara.

Aidha changamoto nyingine alisema wateja walio wengi hawajalizoea soko hilo jipya ambalo awali lilikuwa mkabala na Hoteli ya Peakock Mnazi Mmoja.

Soko hilo jipya hivi sasa limehamishiwa ilikokuwa stendi ya mabasi ya mikoani Kisutu.

“Kuhusu changamoto ni kwamba wafugaji hawapati faida kutokana na biashara kuwa ngumu na wateja hawajazoea soko hili pia,” alisema Ndete.

Katibu wa soko hilo, Bakari Hassan alikiri biashara ya kuku kuwa ngumu, hivyo  aliwataka wafanyabiashara kuwa na subira kwa sababu hali hiyo ipo kila mahali.

“Kweli biashara ni ngumu, lakini naomba wafanyabiashara wawe na subira kwani hali hii ipo kila mahali,” alisema Hassani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles