24.4 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Watanzania wahamasishwa kutumia bidhaa za korosho

Florence Sanawa, Mtwara

KOROSHO ni moja kati ya mazao makubwa ya kimkakati ambapo kitaifa linafanyiwa utafiti na taasisi ya utafiti wa kilimo Tanzania (TARI)  Naliendele iliyopo mkoani mtwara pamoja na mazao mengine kwakushirikiana na vituo vingine 16 vya taasisi hiyo nchini. 

Katika miaka ya hivi karibuni TARI Naeliendele wakishirikiana na bodi ya korosho wameweza kusambaza zao hilo kutoka mikoa mitano hadi kufikia mikoa kumi na saba hali hiyo inaifanya taasisi hiyo kutafuta njia mbalimbali za kuongeza thamani zao hilo ili liweze kubanguliwa nchini na kuongeza pato la mkulima na nchi kwa ujumla. 

Uwepo wa bidhaa hiyo umewezesha wakulima na taasisi mbalimbali nchini kuona umuhimu wa kuwekeza kwenye zao hilo ili kuongeza thamani ya korosho na bibo. 

TARI Naliendele yenye dhamana ya kutafiti zao hilo kitaifa imeweza kuwekeza kwakutoa elimu na kuongeza thamani ya korosho hivyo kuwafanya wakulima kuacha kuuza korosho ghafi.

Naibu waziri wa kilimo Omari Mgumba anasema endapo wanahimiza ubanguaji nchini pia wahimizwe watanzania kupenda kutumia bidhaa zinazolimwa na kuzalishwa nchini kama ilivyo kwenye korosho na mazao mengine.

Anasema utamaduni wa kutumia bidhaa zinazotokana na mazao yanazolimwa nchini kutasaidia kuongeza kipato cha wakulima  kwa kiasi kikubwa.

“Unajua korosho na bibo zinaweza kutumiwa na watanzania na tukawa na afya njema endapo tutahamasika kutumia bidhaa hizi ni wazi kuwa wataalamu wetu wamefanya ubunifu mkubwa hata asiyena meno bado atakunywa maziwa ya korosho,  nitoe wito kwa wawekezaji kuona fursa hii kubwa itakayoowezesha korosho zote zinazolimwa nchini kufanyiwa ubanguaji na kuanza kuuzwa nchini” 

“Sasa ubanguaji umeshuka kwa asilimia 12 pamoja na uwezo wa kubangua kuwa ni asilimia 75 kwa viwanda vilivyopo nchini hadi sasa kuna viwanda 33 vya ubanguaji wa korosho ambapo viwanda 21 tu ndio vinavyofanya kazi”

“Hali hiyo inapelekea uzalishaji kuwa tani 12 kwa mwaka hali ambayo hairidhishi Huku vikundi 200 pekee  vikiendelea  na ubanguaji wa korosho hizo” anasema Mgumba.

Mgumba anasema serikali imesimamia Uboreshaji wa upatikanaji wa malighafi kwa wabanguaji wadogo kwa kuruhusu ununuaji kuendelea kwa mwaka mzima kupitia vyama vikuu  na vya msingi (AMCOS) ambapo awali walishindwa kuingia kwenye ushindani wa minada kutokana na mfumo huo kuwabana.

“Kwa sasa Nchi nyingi ziko kwenye lock down ndio maana tunaangalia mfumo ili wanunuzi waweze kupata bidhaa hiyo kwa njia mbalimbali na pia kutakuwa na masoko mawili ili viwanda vyetu viweze kupata malighafi kwakuwa ubanguaji  unahitajika mkubwa zaidi”

“Kwa sasa zaidi ya asilimia 74 ya korosho zinasafirishwa kwenda Nchini India asilimia 26 zilikwenda Vietnam hii ni hatari wakifunga mipaka tutateteleka kiuchumi ndio maana tunahamasisha ubanguaji na uwekezaji kwa viwanda vidogo na vya kati”

Anaongeza kusema, “Tujenge utamaduni wakula tulichozalisha ifikie wakati kinachozalishwa kiliwe hata hapa nchini tujenge utamaduni wa kula korosho endapo kila mtanzania kwa mwaka akila kilo moja ya korosho tutakidhi soko”

Naye Kaimu Mkurugenzi wa bodi ya korosho Tanzania (CBT) Francis Alfred anasema kuwa lengo ni kuongeza uzalishaji kutoka tani laki 3 hadi kufikia tani milioni moja ambapo wanashirikiana na TARI Naliendele kuzalisha miche na kuisambaza katika maeneo mbalimbali nchini. 

“Na pia tunayomikakati ya kuongeza uzalishaji kwa kiasi kikubwa ndio maana tumekuja na mkakati wa fedha mbegu ili vyama vikuu viweze kuratibu suala la pembejeo ili mkulima aweze kupata bila hata kuwa na pesa na kuwapa vitambulisho ambavyo tunaamini kuwa watapata mikopo na kuondokana na tatizo la mkulima kukosa pesa za pembejeo. 

“Kuongeza thamani ni jambo kubwa ndio maana tunawaunganisha wawekezaji wakubwa wanaokuja mkoani hapa na wabanguaji wadogo ambao wameshindwa kukidhi viwango vya ubora ambapo tunaamini wakiungana itasaidia kutatua changamoto nyingi zaidi” anasema Alfred.

Anaeleza kwamba TARI inafanya kazi nzuri ya kuonyesha ubunifu mkubwa katika zao la korosho ikiwemo kulitangaza na kuongeza wigo wa kilimo kwakushirkiana CBT. 

“Kwakweli tumeona hatua wanayopiga tuko pamoja nao ili kuhakikisha kuwa tunapata wateja kwa bidhaa zote zinazobuniwa na taasisi hiyo ikiwemo juice, jam, wine na kushirikiana nao katika kutangaza bidhaa zote” alisema Francis

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania Dr Fortunus Kapinga  anasema kuwa ili kuongeza thamani ya korosho taasisi hiyo imeweza kubuni bidhaa mbalimbali zitokanazo na korosho. 

Anasema korosho inafungamanisha mazao mbalimbali ikiwemo nanasi, ndizi  na mazao mengine hivyo kitendo cha kuongeza thamani korosho kwa kutengeneza bidhaa mbalimbali itawaunganisha wakulima wengine kwenye biashara hiyo.

“Korosho ina virutubisho vingi ikiwa pamoja na inavitamini C nyingi zaidi Katika korosho ndio maana tunahimiza watu kula na kunywa bidhaa zote zitokanazo na korosho” 

“Korosho ina matumizi mengi wengi hawakuamini kuwa unaweza kula na kunywa korosho leo hii tunayo maziwa ya korosho ambapo unaweza kutumia kahawa, nanasi, ndizi na ngano ukanganya na korosho kupata vitu mbalimbali”

“Pia korosho ina madini ya forfolas, zinki, kalisim, chuma, copa na magnesium, potassium na sidium  na pia  ina vitamin c kwenye bibo mara tano zaidi ya chungwa inasaidia kuleta afya bora” anasema Kapinga

 “Ipo mipango kabambe ya kusambaza huduma hii muhimu kwa afya ili kuweza kuwasaidia watanzania ndio maana tumeweza kusambaza teknolojia mbalimbali za ulimaji wa zao la korosho na kubuni mbegu bora zaidi ya aina 50 ambapo tunaamini kuwa uzalishaji ukiwa mkubwa hata afya zitaboreka kwakutumia zao hili” anasema Kapinga

Kaimu Katibu wa Kamati ya THTU wanawake taifa kutoka chama cha wafanyakazi wa taasisi za elimu ya juu  Tanzania Roseline Massam anasema walikuwa wanajua umuhimu wa korosho lakini hawakujua faida za bibo.

 “Wengi tulijua kuwa korosho ni muhimu sana hatukujua kuwa bibo linafaida kubwa sana na hatukujua kama bibo lina vitamini c mara tano ya chungwa kutokana na kuadimika kwa vidonge vya vitamini c ipo haja ya kuhamasisha wananchi kuanza kutumia bidhaa zitokanazo na bibo ili kuweza kupata vitamini hiyo” 

Nae Dativa Donard kutoka katika kamati hiyo anasema kuwa yeye ni moja kati ya watu walioitikia wito wa kulima korosho kwa mkoani  Morogoro lakini hakuwa na elimu kuhusu zao hilo ambapo amepata elimu anayoamini kuwa itaboresha kilimo katika shamba lake. 

“Kwakweli mimi ni mkulima wa korosho lakini sikujua kama natakiwa kutumia dawa kwenye mikorosho lakini kutoana na elimu hii fupi imenijenga na kunipa elimu kubwa sana”

“Nilijua korosho zinaliwa tu sikujua kama zinaweza kutoa jam, maziwa, kashata, chapatti na maandazi kwangu ni jambo geni sana elimu hii ikitolewa kwa inaoweza kuongeza matumizi ya bidhaa hiyo”

Kwa upande wake Asia Rubeba mhaziri msaidizi chuo kikuu Dodoma kitendo cha korosho kufanyiwa ubunifu mkubwa kitawezesha fursa nyingi kujitokeza hasa wakati huu ambao nchi yetu imeingia katika uchumi wa kati lazima msingi mkubwa uwe ni uwekezaji.

“Uwepo wa hiki kituo unaweza kutumika katika kunufaisiah wanawake ambao wanauwezo wa kupokea fursa mbalimbali ikiwemo uwekezaji kwa kusimama na kufanyakazi kwa bidii katika uzalishaji wa mazao mbalimbali na kuongeza thamani ya mazao hayo ikiwemo korosho”

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles