27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wataalamu wa Mipango watakiwa kutenga bajeti jumuhishi ya malezi

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Serikali imewaagiza Wataalamu wa Mipango na Uratibu katika Sekretarieti za Mikoa kuhakikisha wanatenga bajeti za utekelezaji wa Programu Jumuishi ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (MMMAM) ili kufanikisha malengo ya uanzishwaji wa programu hiyo.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dk. Dorothy Gwajima ametoa rai hiyo akifungua mafunzo ya siku tatu ya utekelezaji wa Programu hiyo kwa Maafisa Maendeleo ya Jamii, Ustawi wa Jamii, Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mipango na Uratibu wa Sekretarieti za Mikoa na Wadau jijini Dodoma.

Waziri Dk. Gwajima amesema katika bajeti zijazo itabidi uhakiki wa bajeti ufanyike ili kubaini kama bajeti ya utekelezaji wa Programu hiyo umezingatiwa.

“Baada ya mafunzo haya Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mipango na Uratibu muende mkatusaidie kuona namna ambavyo afua za Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto zitaingizwa kwenye bajeti ya Serikali katika ngazi ya Mikoa na Halmashauri ili kuimarisha utekelezaji katika ngazi ya msingi,” amesema Dk. Gwajima.

Naye Mkurugenzi wa Maendeleo ya Jamii Patrick Golwike, akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dk. John Jingu, amebainisha kuwa mafunzo hayo ni muendelezo wa jitihada za Wizara na Wadau kuhakikisha utekelezaji wenye ufanisi wa programu hiyo.

“Bila kujenga uelewa kwa watendaji hawataweza kufikia malengo ya programu hii hivyo, lengo ni kujenga uwezo wa wataalamu kwenye kutenga bajeti ambapo wataalamu 124 tayari wameshafikiwa, wakiwemo waandishi wa Habari,” amesema Golwike.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Children in Crossfire, Craig Ferla amesema mara nyingi kuna changamoto ya utekelezaji wa Programu hasa ngazi za chini hivyo ni faraja ya pekee kuwa na Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mipango na Uratibu kwenye mafunzo haya.

“Kwa sensa ya mwaka huu idadi ya watoto wenye umri wa miaka 0-8 ni 27% ya Watanzania ambayo ni sawa na watoto milioni 16 hivyo, watoto hawa ni nguvu kazi ya kipekee ya taifa itakayochagiza uchumi wetu kwa namna tusiyoitarajia,” amesema Ferla.

Naye Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu kutoka Mkoa wa Dar es Salaam, Chillah Moses ameishukuru Wizara kwa jitihada zinazofanywa kuhakikisha utengaji wa bajeti ya kutekeleza programu hiyo kwa manufaa ya watoto nchini.

“Inawezekana wengi wetu tulikuwa hatulichukulii suala la malezi ya watoto kwa uzito unaostahili, lakini Serikali na hata Mhe. Rais mwenyewe anathamini watoto, tunaahidi kuhakikisha bajeti zinapita, safari ya mtoto wa miaka 0-8 inatuhusu,” amesema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles