SARAH MOSES-DODOMA
WAKILI wa Kujitegemea Godfrey Wasonga ametangaza kugombea nafasi ya Urais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), nafasi ambayo kwa sasa inashikiliwa na rais anayemaliza muda wake Fatma Karume.
Amesema endapo atachaguliwa atafanya ushawishi wa kubadilisha Katiba ya nchi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini hapa, alisema endapo atachaguliwa kuwa Rais wa TLS atahakikisha anatumia nafasi yake kufanya ushawishi wa kubadilisha katiba ya Tanzania ili kuondoa sheria kandamizi.
“Ikumbukwe kuwa Katiba tuliyonayo kwa sasa niyamwaka 1964 ,ambayo ilifanyiwa marekebisho mwaka 1977 hivyo kwa sasa haiwezi kuendana na matakwa ya kidunia,” alisema Wasonga
Pamoja na hali hiyo alisema iwapo atapata nafasi ya kuwa rais atakuwa na vipaumbele vitano ambavyo ni kubadilisha Katiba ya TLS kutoka kufanya uchaguzi kwa mwaka mmoja na kuwa miaka miwili.
“Endapo nitachaguliwa pia nitaboresha huduma kwa wanachama hasa katika bima ya afya ili kila wakili awe na bima ya afya ambayo itaweza kumsaidia yeye na familia yake.
“Pia nitakiondoa kipengele cha ulipaji wa ada ambayo hulipwa kila mwisho wa mwaka na badala yake iwe inalipwa mwanzo wa mwaka au wakati wowote na siyo lazima mwisho wa mwaka,” alisema
Alisema katika uongozi wake atakuwa na sera ya Pensheni kwa mawakili ambao watakuwa wamefikia uzeeni ili wawe na kitu ambacho kitaweza kuwasaidia.
“Ada za mawakili zimekuwa zikiongezeka kutoka Shilingi 30, 000 hadi kufikia 50, 000 , na ili uweze kufika katika vikao vya mawakili ni lazima ulipe kiasi cha Shilingi 120,000 lakini katika uongozi wangu nitaishusha hadi kufikia kiasi cha Shilingi 60,000 kama ilivyokuwa awali,” alisema
Wasonga alisema kuwa mchakato wa kuanza harakati za kutafuta kura rasmi leo na uchaguzi unatarajiwa kufanyika Aprili 6, mwaka huu.