26.9 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Wasanii wa kike walio katika mapenzi na wadogo zao

AUNTY34NA GEORGE KAYALA

NICK Cannon na Mariah Carey walifunga ndoa mwaka 2008, licha ya Mariah kuwa na umri mkubwa zaidi ya Nick.

Maisha yao yalikuwa na furaha na kila mmoja alimfurahia mwenzake, huku wakijivunia uhusiano wao uliopelekea ndoa yao kiasi kwamba wakapata watoto wawili mapacha, Monroe na Moroccan Scott Cannon.

Lakini baadaye wawili hao waliachana katika hali ya kutatanisha, kwa kuwa hakuna aliyewahi kuweka wazi kilichosababisha kutengana kwao, ingawa zipo tetesi kwamba wawili hao waliachana baada ya Mariah kudai kuaibishwa na mwanamume huyo baada ya kuwataja kwenye redio wanawake aliowahi kutoka nao kimapenzi.

Maisha ya ndoa yao yamekuwa kielelezo kimojawapo cha kuondoa sitofahamu kwa mastaa mbalimbali kuingia katika uhusiano bila kujali umri, kama kwa baadhi ya wasanii wa kike wa Tanzania wanavyoweka wazi namna wanavyodatishwa na wanaume wenye umri mdogo kwao ambao kiumri ni wadogo zao.

 

Ingawa katika vitabu vitakatifu Biblia na Qur’aan ambavyo ndiyo mwongozo wa maisha ya mwanadamu hakuna maandiko yaliyoweka wazi kama mwanamke kuolewa na mwanaume mdogo ni tatizo, lakini kwa mila na desturi jambo hilo lina ukakasi kama ifuatavyo;.

 

Aunt Ezekiel na Moze Iyobo

Mwigizaji wa filamu za bongo, Aunt Ezekiel, mwenye miaka 29, yupo kwenye mahaba mazito na Moze Iyobo, mwenye miaka 23, ambaye ni mnenguaji wa mwanamuziki wa Bongo Fleva, Naseeb Abdul ‘Diamond’.

 

Kuzidiana huko kwa umri hakukuwafanya washindwe kuendeleza familia yao, kwa sasa wana mtoto mmoja. Aunt Ezekiel anasema: “Kitu muhimu katika uhusiano wetu ni mapenzi tunayopeana ambacho ndicho kitu tunachotaka katika uhusiano wetu na si suala la umri’’.

 

Shilole na Nuh Mziwanda

Mwingine ni Zuhena Mohammed ‘Shilole’, ambaye ni mwimbaji na mwigizaji wa filamu za Bongo, naye amedondokea katika mapenzi ya msanii mwenzake, Naftari Mlawa ‘Nuh Mziwanda’.

 

Umri wa Shilole ni mkubwa kuliko wa Mziwanda, lakini ukubwa wa umri huo hauwazuii kujivunia mapenzi yao na kufanya mambo yao mengine kama kawaida, ingawa mara kwa mara mashabiki wao wamekuwa wakiwapigia kelele kuhusiana na umri wao, lakini majibu ya Shilole ni kwamba; “Sikushawishiwa na mtu kumpenda Nuh Mziwanda, bali moyo wangu ndiyo ulimpenda na hakika ananidatisha siwezi kutengana naye kwa kuwa ni mwanamume kama walivyo wanaume wengine,” hayo ni maneno ya Shilole.

 

Riyama Ally na Idd Mwalimu

Mwigizaji mwingine ni Riyama Ally, huyu humwambii chochote kwa msanii wa muziki wa kufokafoka (hip hop), Idd Mwalimu Mzee, aliyemchumbia hivi karibuni.

 

Ingawa Riyama anadaiwa kumzidi mpenzi wake huyo kwa miaka saba, lakini umri huo haumkatishi tamaa mwigizaji huyo, ambaye muda wote amekuwa akiweka wazi kwamba wamepanga kufunga pingu za maisha.

 

Witness na Ochu Sheggy

Rapa mkali katika kunengua na kuimba, Witness Mwijage `Witness’ pamoja na mpenzi wake, Ochu Sheggy, ambaye naye ni msanii wa muziki wa kizazi kipya, wapo katika mapenzi mazito bila kujali tofauti ya umri wao.

Witness amemzidi umri Ochu, lakini mwenyewe amekuwa akipuuza suala la umri, huku akiweka msisitizo kwamba; “Nasema umri siyo tatizo, nawashangaa wanaofuatilia suala hilo, kwani hawawezi kunitoa katika mapenzi yangu kwa kuwa tunapendana hatuishi kwa ukubwa wa umri.

Kwa nyakati tofauti wasanii hao walieleza kwamba hawakulazimisha kuingia katika uhusiano walionao kwa sasa, hivyo wanawataka mashabiki wao wakubaliane nao na waachane na dhana kwamba lazima waolewe ama kuwa na uhusiano na wanaume wanaowazidi umri.

 

Chris Mauki

Mmoja wa wanasaikolojia, Chris Mauki, anasema endapo mwanamume aliye katika uhusiano ama anaishi na mwanamke aliyemzidi umri ataruhusu kusikia maneno ya jamaa, ndugu na marafiki, inaweza kumuathiri, lakini kama hatasikiliza hatakuwa na tatizo lolote.

 

“Kinachoangaliwa hapa ni upendo, siyo umri, suala la mapenzi ni makubaliano ya watu wawili, ni wazi kwamba kabla ya penzi hilo walikutana na kuambizana, na wakawekana sawa juu ya umri wao, hivyo mtu mwingine hapaswi kuingilia mapenzi yao,’’ alieleza Mauki.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles