27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wasanii kutumia akaunti za Youtube bure

Na Grace Semfuko, MAELEZO, Dar es Salaam

Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Hassan Abbasi amesema Wizara yake, Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, pamoja na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), wameshakubaliana kubadilisha Kanuni ili wasanii na wadau wengine wa maudhui yasiyohusisha uchakataji wa habari waweze kurusha kazi zao kwenye akaunti zao binafsi za YouTube bila kufanya usajili na malipo kwa TCRA.

Akizungumza na Viongozi wa Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF) na vyama vinavyounda shirikisho hilo Jijini Dar es Salaam leo, Dk. Abbasi amesema hatua hiyo imekuja kufuatia kuona umuhimu wa kuwanufaisha Wasanii na kukuza Sanaa nchini.

“Tumefanya mazungumzo na wenzetu wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari pamoja na TCRA kuhusu maudhui ya Tv za mtandaoni, tumeona kuna tofauti kubwa sana kati ya Habari na Sanaa, hivyo tutaboresha kanuni, tumeona eneo hili la Wasanii linapaswa kufanya kazi zao bure, sasa nafurahi kuwaambia kuwa kuanzia sasa wasanii wawe wa muziki au filamu changamoto hii imefika mwisho,” amesema Dkt Abbasi.

Kuhusu maslahi ya kazi za Wasanii zinazorushwa kupitia vyombo mbali mbali vya habari, Dkt. Abbasi amesema, Wizara yake kupitia taasisi zinazosimamia Wasanii ikishirikiana na TCRA wanaendelea kupitia na kuanzisha mfumo wa kuangalia namna ya kazi zao zinavyorushwa kwenye vyombo hivyo ili waweze kulipwa kwa jinsi zinavyorushwa.

“Wizara kupitia Taasisi ya Haki Miliki Tanzania (COSOTA) na wenzetu wa TCRA tunaendelea kukamilisha mfumo wa kuangalia namna ya kazi zenu zinavyoenda katika vyombo vya habari, mfumo huu unalenga kuwanufaisha Wasanii na tayari TV na Redio nyingi wamekubaliana na jambo hili,” amebainisha Dkt Abbasi.

Aidha aliwataka Wasanii kutumia maeneo na mazingira ya uhalisia wakati wa kurekodi kazi zao ikiwa ni pamoja na kutangaza miradi ya ajenda za kitaifa lengo likiwa ni kutafuta fursa za wageni kutembelea maeneo hayo ili kukuza uchumi wa taifa kupitia utalii.

“Tuna miradi mikubwa tunaifanya hapa nchini na kwenye hifadhi zetu za wanyama na kwingineko mnakodhani ni vizuri mkatangaza, tumieni “location” kama zile kutangaza fursa za utalii katika nchi yetu” amesema.

Wakati huo huo, Dk. Abbasi amewataka Wasanii ‘kuacha kiki’ na kutumia taaluma zao vizuri katika kutangaza kazi zao badala ya kuchafuana kwenye mitandao ya kijamii na kueleza kuwa kwa kufanya hivyo wanaondoa uaminifu kwa jamii ambao wameujenga kwa gharama kubwa.

“Wote mmeona yaliyokuwa yakiendelea kwenye mitandao ya kijamii siku za karibuni, sasa ile inaua sanaa, leo hata makampuni yaliyoanza kuwa na imani kibiashara na wasanii wameanza kusita tena, heshimuni sanaa ni maisha ya wengi na hii itawajengea heshima badala ya kutumia kiki za kuchafuana” ameongeza Dk. Abbasi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles