24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Wapewa mbinu kupambana na ubadhirifu vyama vya ushirika

Na Mwandishi Wetu-Pwani

MWENYEKITI wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Dk. Titus Kamani, amewahimiza wakurugenzi wa halmashauri za wilaya, miji, manispaa na majiji kuwawezesha maofisa ushirika waliopo katika maeneo hayo ili waweze kusimamia vyama vya ushirika.

Dk. Kamani alitoa wito huo juzi wakati wa Mkutano Mkuu Maalumu wa wanachama wa Chama cha Ushirika cha Sangasanga Amcos, Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani.

Mkutano huo uliitishwa na kusimamiwa na Mrajis Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Pwani, Angela Nalimi, baada ya kuibuka malalamiko ya wakulima waliokusanya korosho kupitia chama hicho.

“Wakurugenzi wawezesheni maofisa ushirika walioko katika maeneo yenu kwa kuwapatia vitendea kazi ili waweze kusimamia vyama vya ushirika na muwaruhusu kutekeleza majukumu yao waliyopangiwa kwa mujibu wa ajira zao,” alisema Dk. Kamani.

Aliwataka wasimamizi wa vyama vya ushirika wakiwemo warajis wasaidizi wa mikoa na maofisa ushirika kutekeleza majukumu yao ipasavyo katika kusimamia vyama ili kuepuka migogoro na ubadhirifu.

 “Tunataka kuhakikisha tunaondoa migogoro inayojitokeza katika baadhi ya vyama vya ushirika, na tunaowategemea kufikia azma hii ni warajis wasaidizi wa mikoa na maofisa ushirika walioko katika Halmashauri. 

“Tekelezeni majukumu yenu ipasavyo katika kusimamia vyama ili kuondoa migogoro na ubadhirifu,” alisema Dk. Kamani.

Aliwaomba wakuu wa wilaya na mikoa kushirikiana na Tume ya Maendeleo ya Ushirika katika kuwachukulia hatua wabadhirifu wa mali za vyama vya ushirika ili kuvifanya kuwa endelevu na kuwasaidia wanachama.

Akizungumza katika mkutano huo, Kamishna wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Mudhihir Mudhihir, aliwataka viongozi wa ushirika kujiepusha na tabia za udokozi, ikiwemo wizi na ubadhirifu wa mali za chama cha ushirika.

“Kama huwezi uongozi na una tabia za udokozi, usiombe nafasi ya uongozi katika chama cha ushirika,” alisema Mudhihir.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles