24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

‘WANAWAKE NGUZO ZA FAMILIA’

Na PENDO FUNDISHA-MBEYA


BAADHI ya wanawake wa Kijiji cha Ilaji Kata ya Shemwengo wilayani Mbarali, wamesema licha ya jitihada za Serikali na mashirika mbalimbali kupinga ukatili wa kijinsia, matukio hayo yameendelea kushamiri katika jamii inayowazunguka na kuchangia kukwama shughuli za maendeleo.

 

Wakizungumza na MTANZANIA kwa nyakati tofauti juzi, wanawake hao ambao wanajishughulisha na shughuli za kilimo cha mpunga na mahindi, wamesema baadhi ya wanaume wamewafanya wake zao kuwa walezi wa familia na wao wakifanya starehe hasa wakati za mavuno.

Walisema wanawake wamekuwa nguzo za familia kwa kipindi kirefu na kwa kiasi kikubwa cha mazao wanayozalisha huishia kulisha familia na baadhi huuzwa ili kupata fedha kwa ajili ya kusomesha na kununua mavazi kwa watoto.

“Tunafanyakazi ngumu ili kupata kipato kwa ajili ya familia, lakini hatuendi mbele kimaendeleo kwani waume zetu wamekuwa wakishinda vilabuni na hata fedha za kunywa pombe zinatoka kwetu, mbaya zaidi ni pale wakati wa mavuno wanaume ndio wanaotafuta masoko na wakipata pesa hutokomea nazo,” alisema Zainabu Sidiko.

Mariamu Mwakilindwa, Elizabeth Martini na Jamila Juma, walisema jamii hiyo inahitaji kuelimishwa kwani kama itaendelea hivyo kijiji hicho kitabaki kuwa masikini na kila siku wananchi watakuwa wanahitaji msaada kutoka kwa wafadhili na serikalini.

“Wakati mwingine mwanamke hushawishika na kujiingiza kwenye vitendo vya ngono kwa kutembea na wamiliki wa mashamba makubwa hususani kwa wale wanaofanya vibarua, huku wengine wakilazimika kufanya hivyo ili wapate fedha za kununua mbolea au mbegu,” alisema Anna Mwakabonga.

Hata hivyo, walitumia nafasi hiyo kuziomba taasisi na mashirika binafsi kufika na kutoa elimu kwa jamii husika ili ibadilike kwani wanaamini kama mwanamume mmoja kati ya watano ataelimika basi vitendo vya ukatili wa kijinsia vitapungua pamoja na mfumo dume kuondoka.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles