31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wanaoozesha binti zao kimya kimya wafuatiliwe

KHAMIS SHARIF – ZANZIBAR

KUANZIA Novemba 25 hadi Desemba 16 ya kila mwaka, dunia huadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.

Hii ni kutokana kwamba kuna vitendo vingi vya udhalilishaji wanavyofanyiwa wanawake na watoto na hivyo kukosa haki zao za msingi.

Sababu ya kuadhimisha siku hiyo ni kufanya mapitio na tathmini ya kuweza kujua changamoto na mafanikio katika suala la kupiga vita udhalilishaji duniani.

Siku 16 za kupinga ukatili zinalenga kupiga vita unyanyasaji na kuimarisha usawa wa kijinsia ndani ya jamii.

Kila mmoja anatakiwa kuzingatia sababu za kuwapo kwa siku hiyo, ili kuweza kujumuika pamoja na kuhakikisha mapambano dhidi ya udhalilishaji yanafanikiwa kivitendo na si kuhubiri na mwishowe hali hiyo kuendelea.

Hii ni siku ambayo duniani kote huadhimishwa, ambapo Serikali, mashirika na taasisi mbalimbali zinazopiga vita udhalilishaji, huelimisha jamii kutambua  athari za udhalilishaji na jinsi gani zinavyoweza kudumaza maendeleo ya taifa.

Kama zilivyo siku nyengine, maadhimisho ya siku hizi mwaka huu zilibeba ujumbe usemao: ‘Tulinde Nguvu Kazi Tumalize Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji wa Kijinsia Katika Sehemu za Kazi.’

Ujumbe huu unatupa picha kwamba udhalilishaji wa kijinsia upo kila pahala na si ngazi ya kifamilia tu kama ilivyozoeleka hapo awali.

Ikiwa Zanzibar ni moja ya nchi ambazo zinapinga hali hiyo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto, inaendelea kutoa elimu kila eneo kuanzia ngazi ya mikoa, wilaya, hadi majimbo na shehia ili kuhakikisha wanajamii wanaelewa nini maana ya udhalilishaji na kuweka mikakati madhubuti ya kuutokomeza hali hiyo nchini.

Maadhimisho hayo ni chachu ya kutokomeza ndoa kwa wanafunzi na kuwaacha waendelee na masomo yao ili kujipatia maendeleo hapo baadae.

Ikumbukwe kuwa ndoa za utotoni ni tatizo kubwa linaloikabili jamii, jambo ambalo linasababisha kukosa haki zao za msingi.

Wakati Serikali ikibuni mbinu za kutokomeza tatizo la ndoa kwa watoto, wazazi nao wanabuni mbinu ya kuwaoza kimya kimya.

Hii ni tabia ambayo inapaswa kukomeshwa haraka iwezekanavyo kabla haijakomaa, ikiachwa iendelee Taifa halitakuwa na maendeleo yanayokusudiwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles