27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wanaokula vyakula vya kusindika hatarini kupata saratani ya damu

AVELINE KITOMARY Na BATROMAYO JAMES (DSJ) -DAR ES SALAAM

DAKTARI bingwa wa magonjwa ya damu kutoka Taasisi ya Ocean Road (ORCI), Hamisa Iddi, amesema watu wanaokula vyakula vya kusindika wako hatarini kupata ugonjwa wa saratani ya damu.

Awali mwaka 2018 watafiti nchini Ufaransa walisema kuna uhusiano kati ya vyakula vilivyosindikwa na maradhi ya saratani ambapo waliainisha vyakula ikiwemo keki, kuku na mikate kuwa vinasindikwa sana.

Utafiti uliofanywa kwa watu 105,000 umeonyesha kuwa vyakula hivyo huliwa zaidi, hivyo walaji wako hatarini kupata saratani.

Akizungumza na MTANZANIA katika mahojiano maalumu jana Dar es Salaam, alisema hatari hiyo inatokana na vyakula hivyo kuwa na kemikali.

“Kuna vitu ambavyo vinaongeza hatari au uwezekano wa kupata saratani kama vile mionzi, mafuta ya petroli, wadudu wa virusi na bakteria.

“Vyakula vinavyohifadhiwa kwenye makopo vinaongeza uwezekano wa kupata saratani kutokana na kemikali na pia inaweza kutokea bila sababu.

“Mwili wa binadamu ili ufanye kazi vizuri unatakiwa uwe na ‘balance’ kati ya vitu vinavyozalishwa mfano kama wakati wa uzalishaji vingine vife, visipokufa vikazalishwa tu vinaweza kuleta matatizo,” alisema Dk. Hamisa.

Alisema saratani ya damu inaendelea kuongezeka ambapo katika kliniki kwa wiki wagonjwa wanaohudhuria ni 40 huku kanzidata ya hospitali ikionyesha wagonjwa 270 wanatumia dawa kwa mwezi.

“Kwa wastani wagonjwa wapya wa saratani ya haraka ya damu kwa wiki ni watano hadi sita na hii ni ile saratani inayoathiri kwa haraka kuliko ile inayoathiri muda mrefu, hii mgonjwa anaweza kukaa nayo muda mrefu.

“Saratani ya damu inayokuja haraka inafanya seli za mwili kubadilika haraka, hivyo mwili unashindwa kufanya chochote na mgonjwa kushambuliwa na maradhi mengi,” alieleza Dk. Hamisa.

Aidha alisema kuwa saratani ya damu pia huwa inawashambulia watoto huku uwekano wa watoto kupona aina hiyo ya saratani ni mkubwa.

“Wapo watoto wanaopata saratani pia sababu zikiwa ni ‘genetic’ za kuzaliwa nazo, athari zinatokea akiwa tumboni, lakini watoto uwezo wa kupona ni mkubwa endapo watapata matibabu stahiki mapema,” alisema Dk. Hamisa.

Alisema huduma ya upandikizaji wa uloto inayotarajia kuanzishwa hivi karibuni nchini, itakuwa na nafasi kubwa katika kuokoa maisha ya wagonjwa wa saratani ya damu kwani ni tiba.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles