NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM
MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu amesema serikali haitawafumbia macho wanaoingiza bidhaa zisizo na ubora ambapo inapambana kudhibiti uingizwaji wake.
Amesema kutokana na kero hiyo ya muda mrefu atazungumza na Shirika la Viwango Tanzania (TBS), ili kujadili ni kwa jinsi ya kukomesha mianya ya uingizwaji wa bidhaa hizo.
Akizungumza jijini Dar es Salaam juzi katika hafla ya uzinduzi na utoaji tuzo wa Kampeni ya Fahari ya Tanzania kwa bidhaa 50 bora zinazozalishwa na wazalishaji, wajasiriamali wadogo wa ndani iliyoratibiwa na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) na Shirika la Viwango Tanzania (TBS).
“Serikali kwa kushirikiana na TBS, itahakikisha inapiga marufuku ya uingizwaji wa bidhaa hizo ambazo zimeonekana kudumaza uchumi wa nchi pamoja na kuchangia madhara ya kiafya kwa walaji.
“Aidha naunga mkono kampeni hii kwanio itaongeza nafasi za ajira sanjari na kuweka Tanzania katika ramani ya soko la dunia ambapo pia itaongeza thamani ya bidhaa zetu kama ilivyo China ambayo leo hii inasifika kwa uzalishajj na matumizi ya bidhaa zao wenyewe,” alisema.
Kwa upande wake Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage, alitoa agizo kwa kila kampuni kuwa na chapa yake ambayo itahakikiwa na mamlaka husika nchini ili kuongeza ushindani.