31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wanaofunga umeme watakiwa kuwa na vibali

picha-na-3Na TERESIA MHAGAMA- MANYARA

MAKANDARASI wanaofunga nyaya za umeme majumbani, wametakiwa kuwa na vibali kutoka Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).

Hayo yamesemwa jana na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk. Medard Kalemani, wakati wa ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini katika wilaya ya Babati na Mbulu mkoani Manyara.

“Baadhi ya makandarasi wanaofanya ‘wiring’ wamekuwa wakitoza gharama kubwa ya kutoa huduma hiyo na matokeo yake inapelekea wananchi kuchelewa kuunganishiwa umeme.

“Baadhi ya makandarasi wamekuwa wakifanya kazi hiyo chini ya viwango na kupelekea matatizo mbalimbali kwa wananchi ikiwamo nyumba kupata hitilafu za umeme na kusababisha majanga kama ya moto.

“Kwa hiyo atakayetaka kuunganisha umeme kwenye nyumba, lazima awe na kibali cha Tanesco na yeyote atakayekiuka agizo hili atachukuliwa hatua za kisheria,” alisema Dk. Kalemani.

Wakati huo huo, naibu waziri huyo aliwaagiza watendaji wa Tanesco kutoa elimu kwa wananchi kuhusu faida ya kutumia kifaa kijulikanacho kama Umeta (Umeme Tayari) ambacho huwasha umeme ndani ya nyumba bila mteja kulazimika kuingia gharama za kufunga nyaya za umeme ndani ya nyumba.

“Kifaa hiki gharama yake ni shilingi 36,000 tu na kinaweza kutumika kwenye nyumba ya chumba kimoja hadi vitano.

“Kwa hiyo Tanesco mnapaswa kutoa elimu kwa wananchi ili wakitumie kifaa hicho,” alisema Dk. Kalemani.

Pia aliwaagiza watendaji hao wa Tanesco kupeleka wataalamu wawili katika sehemu zenye uhitaji mkubwa wa umeme ambazo kuna shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii ili kusogeza huduma kwa wananchi badala ya wananchi hao kuwafuata Tanesco.

Awali, akizungumzia upatikanaji wa umeme mkoani Manyara, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Raymond Mushi, alisema katika kipindi cha Julai hadi Septemba mwaka huu, Tanesco wameunganisha umeme kwa wateja wapya 1,919 ingawa lengo ni kuunganisha wateja 825.

Kuhusu miradi ya usambazaji umeme vijijini katika awamu ya pili itakayokamilika Oktoba 15, mwaka huu, Mushi alisema miradi hiyo itanufaisha vijiji 96 vikiwamo vijiji 56 vya wilaya ya Babati, Mbulu itakuwa na vijiji 7, Hanang vijiji vinane na Simanjiro ni vijiji 15.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles