24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

WANANCHI NAO WAKAMATWA UPELELEZI KIFO CHA AKWILINA

NA EVANS MAGEGE

KAMISHNA wa Operesheni na Mafunzo  wa Jeshi la Polisi, Nsato Marijani, amesema askari kadhaa na baadhi ya wananchi bado wanashikiliwa kwa upelelezi wa mauaji ya Mwanafunzi wa Chuo cha Usafirishaji cha Taifa (NIT), Akwilina Akwilini.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon Sirro, Marijani, alisema suala hilo lina kesi mbili ambazo ni kuandamana kinyume cha sheria pamoja na kifo cha binti huyo.

“Suala la Akwilina lina kesi mbili tofauti, kuna kesi inayohusu waliondamana kinyume cha sheria na baadhi yao wameshafikishwa mahakamani na wengine watafikishwa mahakamani, kesi ya pili ni mauaji ya Akwilina, suala hili wahusika bado hawajafikishwa mahakamani kwa sababu upelelezi bado unaendelea.

“Taarifa za awali zilisema watu kadhaa walikamatwa pamoja na askari kwa sababu maelezo hayo yalikuwa ni ya muhimu watuambie ni nini kilichotendeka kama sehemu ya upelelezi na wala haina maana wale waliokamatwa pale ndio waliotenda hilo kosa, katika kupeleleza kesi tunakamata na kuwahoji watu wengi na katika kesi tunajua nani mhusika na tumchukulie hatua kali,” alisema.

Marijani alisema kifo cha Akwilina kingeweza kuzuilika endapo watu wasingeandamana kinyume cha sheria.

“Tukumbuke tukio hili lilianza baada ya watu kufanya maandamano kinyume cha sheria na wakapambana na polisi ambao  walikuwa wanahakikisha kwamba sheria inafuatwa.

“Katika tafrani ile polisi walishambuliwa na polisi wawili kujeruhiwa kikatokea kifo cha Akwilina, somo tunajifunza hapa ni kwamba hili lingeweza kuzuilika kama watu watafuata sheria. Kama yatafanyika maandamano kwa mujibu wa sheria hakutakuwa na tafrani na vyombo vya ulinzi na usalama,” alisema.

VIFO MAKADA CHADEMA

Akizungumzia vifo vya makada wawili wa Chadema waliouawa kikatili hivi karibuni, alisema wanawashikilia watu wanne kwa tuhuma za mauaji ya Katibu wa chama hicho Kata ya Hananasif, Daniel John.

Pia alisema watu 10 wanawashikilia kwa tuhuma za mauaji ya Diwani wa Kata ya Namwawala, Godfrey Lwena.

Alisema vifo vya makada hao havina uhusiano wa mambo ya siasa na alifafanua kuwa kifo cha John kinahusiana na masuala ya madaraka huku kifo cha Lwena kinahusiana na migogoro ya ardhi.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles