28.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

Wananchi Dar, Pwani wawasilisha malalamiko 391 Wizara ya Ardhi

Na Beatrice Kaiza, Mtanzania Digital

Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imepokea malalamiko 391 kutoka kwa wananchi wa Halmashauri tano za Mkoa wa Dar es Salaam na hoja tatu kutoka Mkoa wa Pwani katika wilaya za Kibaha na Kisarawe.

Hayo yamebainishwa Dar es Salaam Juzi na Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dk. Allan Kijazi, ambapo amesema kuwa ameunda timu ya Watalaamu kutoka Makao makuu ya wizara kwa ajili ya kusikiliza migogoro hiyo ya ardhi.

Amesema timu hiyo itaanza kazi kwenye kipindi cha wiki moja kuanzia Septemba Mosi hadi 5, mwaka huu.

“Temeke yalikuwepo malalamiko 41, Kinondoni 144, Kigamboni 39, Ubongo 86, Ilala 78, Kibaha na Kisarawe malalamiko 3 ukijumilisha haya unapata malalamiko 391,” amesema Dk. Kijazi.

Pia amesema kamati ambayo aliunda ilifanya uchambuzi wa kina na kubaini changamoto ambazo zinahitaji kikao cha usuluhishi, ufunguaji wa mipaka, madai ya fidia, upangaji na umilikishaji.

Dk. Kijazi amesema miongoni mwa kazi zilizofanyika ni ukaguzi wa maeneo 36 kati ya 38 yenye changamato za uvamizi, upimaji na kubainisha mipaka.

“Wananchi 191 wamepewa majibu kwa kuandikiwa barua kuhusu uamuzi au hatua zinazopaswa kuchukuliwa,” amesema Kijazi.

Aidha, amsema kamati imebaini uwepo wa changamoto kwenye maeneo mahusus yenye migogoro ya muda mrefu mathalani mradi wa kwembe na eneo la kitalu ‘E” Goba Manispaa ya Ubungo.

Amesema zoezi la kutatua migogoro ya ardhi katika mkoa wa Dar es Salaam ni endelevu ili kuhakikisha maamuzi kuhusu malalamiko yaliyowasilishwa imefikia mwisho.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles