Na Anna Ruhasha, Mwanza
Mradi wa maji uliofikia asilimia 90 umeshindwa kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama katika Halmashauri ya Buchosa wilayani Sengerema mkoani Mwanza na kuwafanya wakazi wa eneo hilo kuendelea kutaabika.
Baadhi ya wananchi katika Kijiji Cha Kamisa kilichopo kata ya Kasisa, Amina Rashidi na Joshua Kulwa wakizungumza kwa niaba ya wenzao wamesema kuwa licha ya kuwepo mradi huo unaotekelezwa na wakala wa maji na usafi mazingira Vijiji ( Ruwasa )wilayani Sengerema mkoani hapa bado wanakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama katika eneo hilo.
“Tunaoimba serikali ikamilishe mradi huu kwa wakati , sisi wakazi wa Kijiji hiki hatuna maji ya bomba tunatumia maji ya visima ambavyo vipo mbali na makazi yetu , tunatembea mpaka kilometa moja hadi mbili kufuata maji , mradi huu ukikamilika utatupunguzia adha hii”wamesema wananchi
Akitoa taarifa za utekelezaji wa mradi huo Meneja wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (Ruwasa ) wilayani Sengerema mkoani hapa Venslaus Mosile amesema kuwa mradi wa maji wa Kamisa ni mradi mdogo unatekelezwa kwa zaidi ya sh milion 200 ambapo ukikamilika utatoa huduma kwa kazi 400 na unategemea kukamilika Oktoba mwaka huu.
” Mradi huu umefikia asilimia 90 katika utekelezaji wake , na haujaanza kutoa maji ,tukisema umefikia asilimia 90 tunamaana kazi zote ngumu tumeisha, kama kulaza mabomba ,tumebakiza kuunganisha tu na kazi hiyo ni ya wiki moja tu na huduma ya maji itanaanza kutolewa ” amesema meneja huyo.
Aidha baadhi wajumbe wa kamati ya siasa Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Erick Shigongo na Katibu wa CCM wilaya Barnabas Nyerembi, wakitoa maoni ya utekeleza wa mradi huo hawakulizishwa na kazi ya utekelezaji wa mradi ambapo wamesema taarifa na muonekano wa mradi bado hauleti matumaini wa kukamilika kwa muda uliopangwa .
Agustine Makoye Mwenyekiti wa Kamati hiyo kwa niaba ya wajumbe wameikataa taarifa hiyo na kumtaka meneja wa Ruwasa kuandaa taarifa sahihi yenye uharisia na mradi huo na kuiwasilisha katika ukaguzi ujao.
“Meneja umesema mradi huu umefikia asilimia 90 lakini hautoi maji,hauoni kwamba taarifa zako si sahihi, haiwezekani wananchi wa hapa wanakosa maji serikali imeleta fedha unaiambia kamati kwamba mradi haujaanza kutoa maji , kwanini ulituleta hapa ? Sisi tunachokitaka ni maji yatoke na sisi kama kamati tunaikataa taarifa yako,”amesema Makoye.