23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Wanafunzi 1,674 wachaguliwa kidato cha tano

RAMADHAN HASSAN – DODOMA

JUMLA ya wanafunzi 1674 kati ya 1,861 waliokuwa wanasuburi chaguo la pili la kujiunga na kidato cha tano, wamepewa nafasi hiyo baada ya kuwa na sifa zinazotakiwa.

Pia wanafunzi 187 wameshindwa kuchaguliwa kutokana na tahasusi (combination) zao kutokuwa na ulinganifu unaotakiwa.

Hayo yalielezwa jana jijini hapa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Selemani Jafo alipokuwa akizungumza na waandishi kuhusu uchaguzi wa wanafunzi katika chaguo la pili.

Alisema kati ya wanafunzi 1,674 waliochaguliwa, 1497 wamepangiwa masomo ya sanaa na biashara wakati 178 watajiunga na masomo ya sayansi na hisabati.

Jafo alisema wanafunzi hao wanatakiwa kuanza kuripoti katika shule walizochaguliwa kuanzia Septemba 2 hadi 16 na kuwa watakaoshindwa kufanya hivyo watakuwa wamepoteza nafasi hiyo.

“Pia nitoe wito kwa wanafunzi 187 ambao wameshindwa kuchaguliwa kwa sababu combination zao ‘haziku-balance’ waombe kusoma kwenye vyuo vya ufundi ambayo vinasimamiwa na Baraza la Vyuo vya Ufundi (NACTE),” alisema.

Hivi karibuni Jafo alitangaza uchaguzi wa wanafunzi wa kujiunga na kidato cha tano awamu ya kwanza na kubainisha kuwa 108,644 ambao ni sawa na asilimia 98.31, walichaguliwa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya ufundi ikiwa ni kati ya wanafunzi 110,505 wenye sifa.

Jafo alisema kati ya wanafunzi hao, 69,356 ambapo wasichana ni 31,809 na wavulana 37,547 wamechaguliwa kujiunga na kidato cha tano ambao ni sawa na asilimia 62.76 ya wanafunzi 110,505 waliokuwa na sifa.

Wanafunzi 35,703 walichaguliwa tahasusi ya Sayansi na Hisabati, ambao kati yao wasichana ni 14,876 na wavulana 20,827 huku wa tahasusi ya Sanaa na Biashara ni 33,653, wasichana wakiwa ni 16,934 na wavulana ni 16,719.

Waliojiunga na shule za wanafunzi wenye ufaulu mzuri zaidi (vipaji maalumu) ni 1,462 ambapo wasichana ni 646 na wavulana 816 huku miongoni mwao wanafunzi  sita ni wenye mahitaji maalumu ambao wasichana ni watatu na wavulana watatu.

Alisema wanafunzi wenye mahitaji maalumu waliochaguliwa ni 157 ikiwa wasichana ni 74 na wavulana ni 86 wakati wanafunzi waliochaguliwa ambao waliosoma chini ya taasisi ya Elimu ya Watu Wazima ni 174 ikiwa ni wasichana 74 na wavulana 100.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles