24.4 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Walimu waonywa kutumia makundi ya WhatsApp

Na NORA DAMIAN-DAR ES SALAAM

WALIMU wa shule za msingi Manispaa ya Ilala, Dar es Salaam, wametakiwa kuacha kutumia makundi ya WhatsApp wakati wa mitihani kuepuka kuingia katika kashfa ya wizi wa mtihani.

Akizungumza jana Ofisa Elimu Msingi Manispaa ya Ilala, Elizabeth Thomas, alisema kashfa ya wizi wa mtihani ni mbaya kwani inamfanya mwalimu aonekane hafundishi.

Ofisa huyo alikuwa akizungumza na walimu kutoka kata za Vingunguti, Tabata, Kimanga, Liwiti, Segerea, Kisukuru, Kinyerezi na Bonyokwa kwa lengo la kuwakumbusha maadili ya kazi hiyo na kupokea kero.

“Tunaona ufahari kwa kutoingia katika kashfa ile (ya wizi wa mtihani), kwani inakufanya usitembee kifua mbele kwamba hufundishi unanunua mtihani.

“Tunatakiwa kuwa makini kwa janga hili lililojitokeza, hakikisheni makundi ya WhatsApp yako salama mtumie kwa faida ya kufundishana, wakati wa mtihani mnastopisha,” alisema Thomas.

Ofisa huyo alisema pia hawatambembeleza mwalimu mzembe na kuwataka wafanye kazi kwa bidii kama wanavyopokea mshahara.

“Ukifika kazini fundisha vipindi vyako vyote unavyopaswa, tupambane na mtoto darasani akipanda juu hajui kusoma na kuandika ni kosa la mwalimu,” alisema.

Kuhusu adhabu za viboko aliwataka walimu wakuu wasimamie utekelezwaji wa adhabu hizo na kuwaonya walimu wasilewe sifa ya kupiga.

Naye Ofisa Utumishi wa Manispaa hiyo, Rwechungura Bweba, aliwataka walimu wakuu kutoa taarifa za watumishi hewa na kutahadharisha kuwa ikibainika kuwapo kwa mtumishi hewa mwalimu mkuu wa shule husika atailipa Serikali fedha alizolipwa mtumishi huyo.

“Walimu wakuu na wasimamizi wa vituo mtoe taarifa za watumishi ambao hawapaswi kupata mshahara kwa mwezi, tusipendeleane mtajiharibia,” alisema Bweba.

Mmoja wa walimu kutoka Shule ya Msingi Tabata, Epifania Njau, aliomba malipo ya likizo yalipwe kwa wakati tofauti na sasa ambapo yamekuwa yakicheleweshwa na kusababisha walimu wengi kuwa na madai hayo.

Naye  Mkuu wa Klasta ya Kimanga, Deusdedit Mazala, alisema ilianzishwa Oktoba 10, 2013 na kwamba inahudumia shule 61 zikiwamo 22 za serikali na 39 za watu binafsi.

Alisema ili kudhibiti utoro wa wanafunzi na walimu wameweka mkakati ambapo kila shule kuna mwalimu maalumu anayeshughulika na utoro tu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles