MOSCOW, URUSI
MAANDALIZI yameanza kwa mkutano utakaowakutanisha wawakilishi kutoka Urusi na Mshauri Mkuu wa Masuala ya Usalama wa Marekani, John Bolton, ambao unatarajiwa kufanyika wiki ijayo mjini Geneva nchini Uswisi.
Taarifa hiyo imetolewa jana mjini hapa na msemaji wa Ikulu, Dmitry Peskov.
Alisema kila kitu kinaonekana kitakwenda vizuri kama walivyopanga.
Taarifa hiyo imekuja baada ya juzi, Waziri wa Habari wa Ikulu ya Marekani, White House, Sarah Sanders, kusema kuwa Bolton atakutana pia na wawakilishi kutoka Israel na Ukraine katika mkutano huo wa Geneva.
“Maandalizi tayari yameshaanza na tuna matumaini kila kitu kitakwenda kama tulivyopanga.
“Utakuwa ni mkutano ambao utajadili masuala mbalimbali, hususan ya kiusalama baina ya mataifa haya mawili,” alisema msemaji huyo.
Kabla ya kutolewa taarifa hiyo, awali Ofisi ya Baraza la Usalama ya Urusi ilitangaza kuwapo kwa mkutano huo baina ya Nikolai Patrushev na Bolton, lakini haikueleza ni wapi na tarehe gani utafanyika.
Hata hivyo, hii si mara ya kwanza kwa viongozi wa ngazi ya juu katika masuala ya usalma kukutana, baada ya Julai 27, mwaka huu, Naibu Waziri wa Usalama, Yuri Averyanov kufanya mazungumzo na Bolton mjini hapa na katika kikao hicho kilichoongelewa zaidi ni ushirikiano baina ya mataifa haya mawili.