25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

WAKUU WA MIKOA, MAKATIBU WAKUU WANOLEWA

Na AGATHA CHARLES

WAKUU wa mikoa 13, makatibu wakuu wanne, ma-naibu katibu wakuu 6, makatibu tawala wanne na viongozi kutoka Jeshi la Wananchi  wa Tanzania (JWTZ) na Magereza wako katika mafunzo ya siku tano katika Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC), Kunduchi, Dar es Salaam.

Wakuu hao na mikoa yao kwenye mabano ni John Mongella (Mwanza), Mrisho Gambo (Arusha) na  Anthony Mtaka (Simiyu).

Akizungumza  wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya nne chuoni hapo jana, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ya Zanzibar, Issa Haji Gavu alisema washiriki 45 wanapatiwa mafunzo ya muda mfupi chuoni hapo.

“Malengo ya chuo ni kutayarisha viongozi kwa ajili ya ulinzi na usalama. Viongozi kufahamu masuala ya ulinzi na usalama ni vyema ili kukabiliana na matishio yoyote yanapofika,” alisema Waziri Gavu.

Alisema katika mafunzo hayo, washiriki watajifunza masuala ya ulinzi na usalama kwa upana wake.

Waziri Gavu, alisema hakuna tishio la usalama bali ni kuandaa viongozi kukabiliana na hali yoyote ya maafa au janga.

Naye mkuu wa chuo hicho, Dk. Matern Lumbanga alisema kozi hiyo itawafundisha washiriki misingi ya uadilifu, masuala ya uongozi wa umma na utendaji wa kila siku wa viongozi.

Mmoja wa washiriki hao, Mtaka alisema kozi hiyo ni nzuri hasa kwa vijana. “Ni kozi ya msingi kwa viongozi, si kozi ya kukosa kwa wenye dhamana hasa vijana na ni muhimu katika kuelekea uchumi wa  nchi yetu na viwanda,” alisema Mtaka.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga (RAS) Mhandisi Zena Saidi, alisema ana matarajio makubwa katika kuelewa masuala ya usalama na kujua viashiria vyake katika mkoa na hata nchi.

Alisema kwa sasa mkoa wake uko shwari katika suala zima la usalama. Washiriki hao wanatarajia kuihitimu mwishoni mwa wiki hii.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles