29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

‘Wakuu taasisi zisizolipa gawio kwa Serikali mwisho wa kazi ni Januri’

Na RAMADHAN HASSANDODOMA

SERIKALI imepokea gawio la Sh bilioni 12.12  kutoka  taasisi, mashirika na makampuni 11 huku Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, akisema taasisi nyingine za umma 172 ambazo hazitawasilisha gawio hadi Januari 23 mwaka 2020, bodi na wakurugenzi watakuwa wamejifuta wenyewe.

Mpaka sasa Serikali imepokea gawio na michango kwa taasisi, makampuni na mashirika ya umma, 79 hivyo kubaki 172 kati ya 187.

Novemba 24 mwaka huu, Rais Dk. John Magufuli akiwa katika Ikulu ya Chamwino jijini hapa alipokea gawio kwa taasisi za umma 54 ambazo kwa ujumla zilitoa Sh trilioni 1.05.

Mara baada ya kupokea Rais  Magufuli alitoa siku 60 kwa wakurugenzi na wenyeviti wa bodi za mashirika, taasisi na kampuni za umma 187  kuhakikisha wanatoa gawio kwa Serikali, kinyume na hapo waondoke wenyewe katika nafasi zao.

Kutokana na agizo hilo la Rais, Novemba 25 mwaka huu, Waziri wa Fedha alipokea gawio na michango la Sh bilioni 2.75 kutoka kwenye   taasisi nne.

Kaimu Msajili wa Hazina Athuman Mbuttuka jana alizitaja baadhi ya taasisi, mashirika na makampuni yaliyowasilisha gawio kuwa  ni  Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) Sh. milioni 100, Chuo Kikuu cha Sokoine  cha Kilimo (SUA) Sh. milioni 100, Jeshi la Magereza Sh. milioni 100, Chuo cha Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (Veta) Sh. bilioni 1, Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (Nacte) Sh. milioni 855, Chuo cha Mipango Sh. milioni 100.

Akizungumza mara baada ya kupokea gawio na michango hiyo, Dk. Mpango alisema Novemba 24 Rais alitumia lugha kali kwa taasisi, makampuni na mashirika ya umma ambayo hazijatoa gawio la Serikali.

Alisema yeye akiwa Mtendaji Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, atahakikisha maagizo yale yanafuatwa.

“Wajibu wenu kama viongozi, sasa labda niseme tena tarehe 24 Novemba Rais alitumia lugha kali lakini  moja alininong’oneza pale pale wakati akipokea gawio  kwamba Waziri acha kuwa mpole.

“Nataka kutumia fursa hii kuwakumbusha wote ambao hawajaleta gawio ama mchango kwenye mfuko Mkuu, makampuni taasisi na mashirika yote ambayo Serikali imewekeza kuwataka kwamba itakapofika saa sita usiku tarehe 23 Januari 2020.

“Kama hawajaleta gawio wala michango ya kuingia katika mifuko mikuu bodi hizo zimevunjwa. Sasa hizo taratibu tutazifuata, watendaji wakuu katika taasisis hizo sijui mimi nateuliwa na nani? Sasa hiyo ndio amri ya Serikali, mchezo umekwisha lazima Tanzania iende mbele.

“Ukitaka upone zamani unapiga klorokwini baada ya saa sita unaenda kucheza huo ndio utaratibu. Mimi nasema kupitia kwenu nyinyi mmefanya kazi nzuri mmeifanya asubuhi yangu imekuwa njema. Natarajia mwaka kesho mtakuwa hapa na mtakuwa pembeni ya Rais na msilete kidogo, leteni nyingi  ili tufanye mambo makubwa zaidi kwa ajilli ya Watanzania maskini,”alisema Dk Mpango.

Alisema kulipa gawio na michango ndio njia nzuri la taifa kuweza kujitegemea katika mambo yake huku akisisitiza ni aibu kwa Waziri wa Fedha na Mipango kwenda kuomba omba kwa wahisani.

“Ninafura hii ndio njia ya Nchi yetu kujitegemea, Waziri wa Fedha kwenda kuomba omba sio jambo zuri, tunadhalilika sana na Rais anatukumbusha nchi yetu ni tajiri hakuna ambazo Mungu ametunyima .

“Tusimpeleke Rais kwenda kuomba mpelekeni kwenda kukopa ili tuje tulipe lakini kwenda kukinga bakuli tufike mwisho,”alisema.

Waziri huyo aliwahakikishia Watanzania kwamba fedha hizo zitatumiwa vizuri kwa ajili ya kuleta maendeleo na kuwasaidia wale ambao ni maskini.

“Niwahakikishie Watanzania tutatumia fedha hii vizuri tutaitumia kwa maendeleo ya Watanzania, subirini muone lile limeli pale Mwanza, angalieni mimi natoka Kigoma miaka iliyopita nilikuwa natumia siku nne sasa nikitoka asubuhi jioni nakula Mgebuka Kigoma,”alisema

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles