31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wakulima Simiyu wapewa tahadhari kutunza chakula

Na Derick Milton, Nyakabindi

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dk. Yahya Nawanda amewataka wakulima mkoani humo, kuhakikisha wanatunza chakula katika kipindi hiki kwani uzalishaji utakuwa mdogo kutokana na hali ya hewa.

Dk. Nawanda amesema kuwa kutokana na mvua kuwa chache na uzalishaji wa mazao kuonekana kuwa mdogo, amewataka wakulima kwa mazao ambayo watavuna kuyatuza kwa ajili ya familia zao wakiwemo watoto.

Mkuu huyo wa mkoa amezungumza hayo jana, akiwa na wakulima kwenye kituo cha umahili cha usambazaji teknologia za kisasa za kilimo TARI Nyakabindi wakati wa siku ya mkulima shambani.

Amesema kuwa kutokana na hali hiyo, wakulima hawana budi kuacha kuanza kuuza chakula, na badala yake wakitunze ili kuweza kukitumia wao pamoja na familia zao kwani uzalishaji utakuwa kidogo.

Amewataka wakulima kutouza chakula chote walichonacho, na badala yake wakitunze ili kije kuwasaidia mbeleni ikiwa kutakuwepo na upungufu wa chakula nchini.

“Niwaombe wakulima wa mkoa wa Simiyu, tutunze chakula ambacho tumezalisha mwaka huu, hali ya hewa siyo mzuri na uzalishaji ni mdogo, hivyo sasa tutunze hiki chakula, tusiuze, tukitunze kwa ajili ya familia zetu,” amesema Dk. Nawanda.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa amewasisitiza wakulima kutumia vyema uwepo wa kituo cha TARI Nyakabindi mkoani humo, kwani kinazalisha teknologia nyingi za kisasa za kilimo ikiwemo mbegu bora.

Amewataka watalaamu kwenye kituo hicho, kuhakikisha wakulima wengi zaidi mkoani humo wanafika kituoni hapo kwa ajili ya kujifunza ikiwa pamoja na kupewa mbegu bora za kisasa ili waweze kuzalisha kwa tija.

Nao wakulima waliohudhulia siku hiyo, wamekipongeza kituo hicho kwani kimewabadilishia maisha kwa kuwafundisha njia bora za kilimo cha kisasa kuliko ilivyokuwa zamani.

Wakulima hao wamesema kuwa uwepo wa kituo hicho, wamenufaika kwa kiwango kikubwa, kwani ujifunza kila wakati namna bora ya kuzalisha kwa tija ikiwa pamoja na kupatiwa mbegu bora zilizofanyiwa utafiti.

“Kama wakulima tumenufaika kwa kiwango kikubwa na kituo hiki tangu kimeanzishwa, tumepata elimu, mbegu bora, tulikuwa tunalima kwa mazoea lakini kwa sasa tunalima kisasa, na kwa tija,” amesema Elia Elisha mkulima.

Hata hivyo wakulima wameiomba serikali kutatua changamoto ambayo inakikabili kituo hicho ya upatikanaji wa maji ya uhakika, kwa kichimba kisima kirefu ambacho kitazalisha maji muda wote.

Naye Mratibu wa uhaulishaji wa teknologia kutoka TARI ukiriguru mkoani Mwanza, Dk. George Sonda, amewasisitiza wakulima katika kipindi hiki ambacho Mamlaka ya hali ya hewa nchini imetangaza kuwepo kwa mvua chache zitakazonyesha, kutumia mbegu zinazozalishwa na kituo hicho ambazo zinastahimili ukame.

Ofisa Mfawidhi wa kituo hicho cha Nyakabindi Isabela Mrema amesema tangu kituo kianzishwe toka mwaka 2021, jumla ya wakulima 3,121 wanawake wakiwa 750 na wanaume 2,371 wamepewa mafunzo ya teknologia za kisasa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles