27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Wakimbizi wanaojishughulisha na siasa makambini wapewa onyo

Na Allan Vicent, Tabora

SERIKALI imewataka wakimbizi waliopo nchini kuacha kujihusisha na harakati za kisiasa katika makazi ya wakimbizi yaliyoko katika maeneo mbalimbali nchini na kwamba wanapaswa kuishi kwa kuzingatia sheria za nchi.

Onyo hilo lilitolewa jana na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, alipokuwa akizungumza  na mamia ya wakimbizi kutoka nchi jirani ya Burundi wanaoishi katika makazi ya wakimbizi ya Ulyankulu yaliyoko wilayani Kaliua mkoani Tabora.

Alisema Tanzania ni nchi ya amani, ndio maana iliwapokea na kuwapa hifadhi ili wakae kwa amani na utulivu na baadhi yao wameshapewa uraia wa  kudumu, hivyo wanapaswa kutii sheria za nchi na kujiepusha na mambo yasiyofaa.

Aliwataka raia wapya wote kutojificha bali wawe huru na kushirikiana na wenzao katika shughuli zote za ujenzi wa nchi yao mpya (Tanzania) huku akiwataka kutoogopa kutaja makabila yao kama ni mhutu ajitambulishe kuwa ni mhutu.

Aidha aliwataka wale wote wanaojihusisha na vitendo vya uvunjifu wa amani ikiwemo ujambazi ikiwemo wanaochokonoa mambo yanayoendelea katika nchi yao ya zamani (Burundi) kuacha mara moja tabia hiyo kwa kuwa hayawahusu.

“Serikali ya Tanzania inawapenda sana, tulieni, acheni kuendesha harakati za kisiasa katika makazi haya, hapa sio mahala pake, mtajiletea matatizo, wale wote mnaotaka kurudi kwenu mlango uko wazi”, alisema.

Simbachawene alimwagiza Mkurugenzi wa Huduma za Wakimbizi, Sudi Mwakibasi kwa kushirikiana na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) kufanya tathmini ya wale wote wanaotaka kurudi kwako ili serikali iandae utaratibu wa kuwarudisha.  

Aidha aliwataka kuwa watulivu huku akibainisha kuwa serikali itaweka utaratibu mzuri kuwapatia huduma zote wanazostahili kama raia ikiwemo kupewa elimu ya uraia ili watambue haki zao.

Kwa upande wake Mwakibasi alimhakikishia Waziri kuwa Ofisi yake ipo tayari kuwasaidia wakimbizi wote wanaotaka kurejea kwao warejee kwa amani na hata serikali mpya ya Burundi imesema kuwa ipo tayari kuwapokea.  

Awali Mkuu wa wilaya ya Kaliua Abel Busalama alimweleza Waziri Simbachawene kuwa wakimbizi waliopo katika Makazi hayo ni wachapa kazi na watiifu, ndio maana wamekuwepo hapo kwa miaka mingi tangu walipoingia nchini mwaka 1972.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles