23.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Wakesha kwenye mvua kuokoa maisha ya mtoto anayeugua saratani

JOSEPH HIZA NA MASHIRIKA

MAELFU ya watu wamejitokeza kupanga foleni ya kujiandikisha kutoa chembe za msingi (stem cells) ili kuokoa maisha ya mvulana mwenye umri wa miaka mitano anayeugua saratani ya damu. 

Mvulana huyo, Oscar Saxelby-Lee, amevutia watu 4,855 nchini Uingereza waliojitokeza waliojitokeza katika zoezi  hilo ili wachukuliwe sampuli zitakazochunguzwa kuangalia iwapo chembe zao hai zinalingana na za mtoto huyo.

Madaktari wanasema mwanafunzi huyo ana miezi mitatu tu ya kumpata mtu atakayejitolea chembe hai nyekundu za damu ili kutibu maradhi mabaya yaliyompata ya saratani inayoitwa kitaalamu Acute Lymphoblastic Leukaemia (ALL).  

ALL ni aina ya saratani ya damu, ambayo inaanza kutokea katika chembe changa nyeupe za damu zilizopo katika uboho wa mfupa.

Mazingira ya hatari yanayoweza kumfanya mtu augue ALL ni pamoja na kukabiliana na miale, uvutaji sigara, uzito mkubwa na kuwa na mfumo dhaifu wa kinga ya mwili.

Tiba kuu dhidi ya ALL ni pamoja na ni ile ya kemikali (chemotherapy). Wagonjwa pia wakati mwingine hulazimika kupata tiba ya mionzi, steroids au upandikizaji wa uboho.

Wazazi wa Oscar, mama Olivia Saxelby na baba Jamie Lee wakazi wa St. John’s, Worcester nchini Uingereza, walianzisha mpango huo wa kutafuta watu wenye chembe zinazofanana baada ya mtoto wao huyo kugundulika kuwa na ugonjwa huo hatari.

Walilenga kupata watu wengi kadiri iwezekanavyo, ambao watajiandikisha kwa ajili ya kujitolea chembe za msingi kama sehemu ya kampeni inayoitwa ‘Mkono kwa Mkono kwa ajili ya Oscar.’


Oscar Saxelby-Lee

Oscar tayari amefanyiwa tiba ya chemotherapy tangu agundulike na maradhi hayo Desemba mwaka jana, lakini anahitaji matibabu ya kina zaidi ili kumtibu. 

Wazazi wa Oscar awali walikuwa na wasiwasi wakati walipoona alama zisieleweka katika mwili wa mvulana wao na Desemba mwaka jana kabla ya kumpeleka hospitali walikoambiwa ana ALL.

Familia baada ya kushauriana na shule yake wakaja na wazo la kushindana na muda huo wa miezi mitatu uliowekwa ili kumwokoa.

Inamaanisha kwamba bila kujitokeza kwa wakati kwa mtu huyo mwenye chemba za msingi zinazofanana na zake ndani ya muda huo, nafasi ya kuishi ya Oscar itatoweka.

Lakini kuonesha namna gani watu walivyoguswa, umati ulijitokeza katika tukio la kujisajiri kutafiti chembe zao ili iwapo zinafanana na za mtoto huyo katika Shule ya Msingi Pitmaston huko Worcester huku mvua kubwa ikinyesha.

Taasisi ya Hisani ya DKMS ambayo iliendesha zoezi hilo la kusaka mtu sahihi wa kujitolea ilisema rekodi yake ya awali ya watu kujitokeza katika tukio moja kama ilikuwa 2,200, ikimaanisha Oscar amepata watu zaidi ya maradufu.  

Mwalimu wa Oscar, Sarah Keating anasema: “Nimekuwa nikifundisha kwa zaidi ya miaka 20 na sijawahi kuona mtoto mdogo akipitia katika kitu kama hiki.

“Unasikia kuhusu watoto kupata saratani na mawazo yanayokujia ni kitu kibaya kwa mtoto, kisha mnatafuta suluhu. Katika kesi kama hii bado hatujasonga mbele vya kutosha, licha ya wingi wa watu uliojitokeza kutupa nguvu, bado tunapambana.”

ALL ni maradhi ya nadra na huathiri watu 650 nchini Uingereza kila mwaka na nusu yao wakiwa watoto. 

Ni maradhi ambayo hujitokeza kwa kasi, ni saratani mbaya sana, ambayo inasababisha idadi kubwa ya chembe nyeupe za damu zisizo imara kuharibika kutoka uboho wenye maradhi.

Chembe nyekundu za damu huendelea kusambaa na kusababisha dalili kama za uchovu, ugumu wa kupumua, ngozi angavu, homa na maumivu ya mfifuopa na viungo.

Oscar alifanyiwa tiba ya chemotherapy mara 20 katika wiki nne.

Mwalimu wa Oscar, Laura Senter (22) anasema kugundulika kwake maradhi hayo, kulikuja kama mshtuko kwa darasa lao kwa sababu ugonjwa wake ulichomoza na kukua kwa haraka mno.

Anasema: “Sikuweza kuamini hilo. Nilimuona kabla ya Siku Kuu ya Krismasi na alikuwa na furaha kama kawaida.

Mama wa Oscar, Olivia, anasema mwanawe amekuwa shujaa wa kweli kipindi chote cha ugonjwa wake.

“Tuliamua kutafuta mtu wa kujitolea chembe, watu karibu 5,000 wakajitokeza. Walipanga mstari huku mvua kubwa ikinyesha na kujaza kumbi mbili za shule wakati wa mwishoni mwa wiki ili kujiandikisha na kupimwa,” anasema.

Watu waliojitokeza kupima chembe zao

Wanasayansi wanaendelea kuchunguza sampuli za watu hao kupata mtu ambaye chembe hai zake nyekundu za damu zinaoana na zile za Oscar ili mwili wake uweze kuzikubali wakati zitakapopandikizwa.

Oscar anahitaji upandikizaji wa chembe za msingi za damu ili kuzijaza upya zile zake mwenyewe, ambazo zimeharibiwa wakati wa mchakato wa chemotherapy. 

Senter anaongeza: “Nilimtembelea Oscar hospitalini mwezi uliopita wakati wa siku yake ya kuzaliwa. Wazazi wote waliokuwapo walimnunulia zawadi.

“Kwa sababu ya chemo alionekana kudhoofu lakini unaweza kuona uhai wake ungalipo ndani yake.”

“Wakati tulipotoka tulijua kwamba tunapaswa kufanya kitu cha kuweza kumsaidia na hili tangazo lililoshuhudia maelfu wakijitokeza ndiyo uamuzi tuliofikia pamoja na wazazi wake,” Senter anasema.

Haijaweza kufahamika bado iwapo madaktari wameweza kupata chembe zinazooana na za Oscar lakini Sarah Gray, Msemaji wa Taasisi ya Hisani ya DKMS anasema ni kazi ngumu kupata chembe aina hizo, ni sawa na kushinda bahati nasibu. 

“Inakanganya, lakini kwa kadiri ya watu wanavyojitokeza kujiandikisha ndivyo nafasi zaidi za kuokoa maisha ya wagonjwa kama Oscar inakaribia.

Miss Saxelby (23) anasema: “Tulihisi hatutaona mwanga mwishoni mwa shimo, wakati tukitazama tabasamu tamu na dhamira ya Oscar, tukaweza kukusanya nguvu pamoja kwa mara nyingine.

“Kuanzia wakati huo wa hofu na mkanganyiko, kama familia tukawa wenye nguvu kwa mara nyingine. Oscar alitukumbusha namna kupambana tena na alivyo jasiri.

“Hajawahi kuonesha udhaifu, wala hakuacha kutushangaza kipindi chote cha nyakati ngumu na kwetu sisi ni shujaa wa kweli.

“Oscar ni mcheshi, mwenye upendo, nguvu na mvulana wa miaka mitano anayepambana na maradhi mabaya ya kutisha kama haya.”

NAMNA UPANDIKIZAJI CHEMBE ZA MSINGI UNAVYOFANYA KAZI 

Kama tiba kwa acute lymphoblastic leukemia (ALL), upandikizaji wa chembe za msingi hufanya kazi kwa kuondoa chembe za damu zenye maradhi au zilizoharibiwa na chemotherapy.

Kuwa na upandikizaji chembe za msingi kunamaanisha mwili unaweza kuhimili dozi ya chemotherapy na matibabu mengine ya saratani.

Wakati wa chemo, seli za saratani zinapoharibiwa na dawa, zile zenye afya ambazo ni lazima kwa viungo vya ndani na mfumo wa kinga nazo hufanya kazi sawa sawa.

Kuwa na mtoaji kunamaanisha kwamba chembe zilizoharibiwa na chemo zinaweza kuondoshwa na nafasi yake kuchukuliwa na chembe za msingi – ambazo zinageuka kuwa chembe nyekundu na nyeupe za damu mara zinapoingizwa mwilini, humsadia mgonjwa kupona haraka kutokana na ‘gruelling therapy.’ 

Chembe za msingi huchukuliwa kutoka sampuli ya damu ya mtoaji, ambao uboho wao unafaa kupandikizwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles