27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

WAJIBU WA MZAZI KWA MTOTO  KISHERIA

Na Christian Bwaya


TUMESHUHUDIA matukio mengi katika jamii yetu ya watoto kunyanyaswa na kudhalilishwa na watu wazima wakiwamo walezi na hata baadhi ya wazazi wasio waadilifu.

Imekuwa kawaida kusikia yatima wakitendewa vitendo vya uonevu baada ya wazazi wao kufariki. Ndugu na jamaa, bila haya, wamekuwa wakifanya uamuzi unaowahusu watoto bila kuzingatia maslahi na haki zao.

Unyanyasaji wanaofanyiwa watoto, wakati mwingine unafanyika kwa sababu wazazi, walezi na hata jamii kwa ujumla hawafahamu wajibu walionao kwa mtoto kisheria. Kutokujua namna mtoto anavyolindwa kisheria kunaweza kwa namna moja au nyingine, kuchochea vitendo hivi.

Katika safu hii, tunakusudia kukuletea dondoo muhimu kama zinavyoainishwa kwenye sheria ya Mtoto Na. 21 ya 2009 iliyotungwa kwa minajili ya kulinda maslahi na ustawi wa mtoto. Sheria hii ilitungwa na serikali yetu kukidhi matakwa ya mikataba ya kimataifa inayomhakikishia mtoto haki zake za msingi.

Kwa mhutasari, sheria hii inalenga kumwekea mtoto mazingira ya kukua na kustawi katika nyanja zote za kimaisha bila kudhalilishwa, kuonewa na kunyanywaswa na jamii ikiwamo familia yake. Ingawa msisitizo ni kumlinda mtoto zaidi, sheria hii pia inafafanua wajibu wa mtoto kwa familia na jamii kwa ujumla.

Labda tuanze na tafsiri ya mtoto. Mara nyingi tumetumia neno ‘mtoto’ kumaanisha mambo mengi kwa wakati mmoja. Kwa mfano, unaweza kushangaa mzee wa miaka 55 anajitambulisha kama ‘mtoto’ wa tatu katika familia yake. ‘Mtoto’ huyu wa tatu, naye anaweza kuwa na ‘watoto’ kadhaa wenye umri wa utu uzima.

Hapa mtoto maana yake ni nini? Mtoto, katika mazingira hayo, ni mtu aliyezaliwa na mtu mwingine bila kujali umri wake. Tafsiri hii inazingatia uhusiano wa mzazi na mwanawe bila kujali umri.

Kadhalika, unaweza kusikia mtu mwenye miaka 40 akidaiwa kufanya mambo ya kitoto. Utoto, kwa mazingira hayo, ni kufanya vitendo visivyoakisi uwezo wa mtu mzima anayejitegemea. Jamii inakuwa na matarajio fulani kwa mtu anayejitambulisha kama mtu mzima. Anatarajiwa kufikiri kwa namna fulani, kufanya vitu kwa namna fulani na hata kuonekana kwa namna fulani.

Inapotokea mtu mzima huyu anashindwa kukidhi matarajio hayo, watu humtazama kwa jicho la ‘utoto.’ Utoto ni sifa mbaya kwa mtu mzima.

Lakini, kidini tunaambiwa “msipokuwa kama watoto wadogo hamuwezi kuurithi uzima wa milele.” Mtoto, katika mukhtadha huu, si sifa mbaya. Tabia za kitoto kimsingi ni sharti muhimu la kumpa mtu sifa za kuuona ufalme wa mbinguni.

Kisaikolojia, mtoto anaweza kuwa na umri wowote ingawa mwenye miaka pungufu ya 12 ana nafasi kubwa ya kufahamika kama mtoto. Sababu kubwa ni kuwa katika umri huo, mtu huyu bado anaendelea kukomaa na kupevuka kiakili, kimwili, kiroho na kimahusiano ni mtoto.

Kwa kuwa tafsiri za ‘mtoto’ na ‘utoto’ zinaweza kuwa na mkanganyiko mkubwa kama tulivyouona hapo juu, sheria hii imetumia kigezo kimoja cha umri kumtambua mtu mwenye sifa za kuitwa mtoto.

Mtoto, kwa mujibu wa sheria hii, ni mtu yeyote mwenye umri wa chini ya miaka 18. Haijalishi amepevuka akili kiasi gani, maadam ana umri usiozidi miaka 18 mtu huyo bado ataendelea kutambuliwa na sheria hii kama mtoto.

Mtu anayekidhi sifa hii amepewa haki na wajibu kisheria kama tutakavyobainisha katika makala inayofuata.

Itaendelea

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles