26.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Wajawazito Zanzibar wapewa somo madhara mitishamba, wakunga wa jadi

KHAMIS SHARIF-ZANZIBAR

MUUGUZI Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Kivunge, Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mwanamvua Said Nassor, amesema wajawazito kukimbilia kwa wakunga wa jadi na kutumia miti shamba, ni baadhi ya sababu ya vifo vingi vyao na watoto.

Kutoka na hali hiyo, amewahimiza wajawazito kujifungulia hospitalini kwani licha ya Serikali kuimarisha huduma za afya, bado wapo wanaoendelea kujifungua kwa wakunga wa jadi na wanapopata matatizo ndipo hukimbilia hospitali.

Akizungumza na MTANZANIA jana ofisini kwake Kivunge, Dk. Mwanamvua alisema sababu nyingine zinazosababisha vifo vya wajawazito ni utapiamlo na kifafa cha mimba.

Alisema mwaka jana hadi Juni mwaka huu, watoto wasiopungua 30 walipoteza maisha katika hospitali hiyo, kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo mama zao kujaribu kujifungua kwa wakunga wa jadi.

“Tatizo ni wajawazito kujifungua nyumbani, licha ya kuendelea kutoa elimu na Serikali kujitahidi kuimarisha huduma za afya, wapo wanaoendelea kujifungua huko,” alisema Dk. Mwanamvua.

Alisema asilimia 90 ya wanawake hubeba mimba wakiwa na umri mdogo na kutumia vyakula visivyo na lishe, jambo linalochangia matatizo kwao na watoto.

“Kujifungua nyumbani kuna changamoto nyingi, wajawazito hutoka damu nyingi na hatimaye wanapofikishwa hospitali huwa wamechoka na inakuwa vigumu kuwasaidia, wengine hutumia miti shamba wakiwa wajawazito.

“Lakini tutaendelea kutoa elimu juu ya athari ya matumizi ya miti shamba, kwa mfano mti unaoitwa mpambawake watu wanaamini unaongeza damu kwa mjamzito, lakini kitaalamu mti huu unasababisha mkojo kuwa mchafu na kupelekea matatizo wakati wa kujifungua,” alisema.

Alieleza kwamba kwa mwezi watoto 10 hadi 15 hupokewa katika hospitali hiyo wakiwa na utapiamlo na upungufu wa damu.

Dk. Mwanamvua alisema kutokana na mazingira hayo, mahitaji ya damu salama hospitalini hapo huwa makubwa. Kwa mwezi zaidi ya chupa 30 hutumika kuhudumia wagonjwa, hasa wajawazito na watoto.

Alisema katika kuhakikisha matatizo hayo yanapatiwa ufumbuzi, madaktari na wauguzi wa hospitali hiyo wanatoa elimu kwa wakunga wa jadi, masheha na wajawazito juu ya umuhimu wa kuvitumia vituo vya afya na hospitali kujifungua.

Dk. Mwanamvua alisema miongoni mwa juhudi nyingine zinazochukuliwa ni kuelekeza nguvu ya elimu ya afya katika vijiji jirani kama vile Matemwe na Nungwi ambako changamoto inaonekana kuwa kubwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles