27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wajawazito wenye msongo wa mawazo hujifungua watoto wenye ukosefu nguvu za kiume

HASSAN DAUDI NA Na LEONARD MANG’OHA

-MITANDAO/DAR 

MSONGO wa mawazo si tu humuathiri mjamzito, pia ni chanzo cha mtoto wa kiume atakayezaliwa kuwa mgumba, kwa maana ya kukosa uwezo wa kumpa mimba mwanamke, utafiti mpya umebaini.

Itakumbukwa awali msongo wa mawazo ulitajwa kuwasababishia wajawazito shinikizo la damu, ugonjwa wa moyo na mtoto njiti (aliyezaliwa kabla ya wiki 37 za ujauzito).

Pamoja na hayo, safari hii, watafiti wa Chuo Kikuu cha Western Australia wamekuja na majibu mapya kupitia utafiti wao mpya uliowahusisha wajawazito 3,000, ukieleza uhusiano uliopo kati mjamzito mwenye hali hiyo na mbegu za kiume za mtoto wake.

Inaelezwa, matukio msongo wa mawazo kwa mjamzito, ikiwamo vifo, kutwangwa talaka au kufukuzwa kazi, humfikia moja kwa moja mtoto aliye tumboni na kuathiri ukuaji wa homoni muhimu za viungo vyake vya uzazi.

Kupata majibu hayo, wataalamu wa taasisi hiyo ya elimu waliwafuatilia watoto wa kiume 643 walipofikisha umri wa miaka 20 na kupima mbegu zao, pamoja na kuwachukulia vipimo vya damu.

Kilichobainika katika uchunguzi wao ni kwamba vijana ambao wazazi wao walikuwa na msongo wa mawazo katika wiki 18 za ujauzito, mbegu zao hazikuwa zimetimia na pia kasi yake ilikuwa chini.

“Tulikuta wanaume ambao wazazi wao walikumbwa na matukio yaliyowapa maisha ya msongo wa mawazo wakiwa na upungufu wa hadi asilimia 36 ya idadi ya mbegu,” anafafanua Profesa wa Afya ya Uzazi katika Chuo Kikuu cha Western Australia na kuongeza kuwa;

“Hata kasi ya mbegu hizo ilikuwa imepungua kwa asilimia 12,”.

Akiyazungumzia matokeo ya utafiti huo, Profesa wa magonjwa ya wanaume katika Chuo Kikuu cha Sheffield, Uingereza, ameonesha kukunwa na utafiti huo akisema ni kweli ubora wa mbegu za kiume unaweza kuathiriwa hata kabla ya mtoto kuzaliwa.

Kwa upande mwingine, utafiti huo unaendana na ule uliowahi kufichua kuwa idadi ya mbegu za kiume zimepungua kwa kiasi kikubwa duniani, ukilinganisha na miaka 80 iliyopita.

Nchini Uingereza pekee, tatizo ni kubwa kiasi kwamba kati ya makundi sita ya wapenzi/wanandoa, moja linakwazwa na tatizo la kutopata mtoto.

Akizungumzia utafiti huo, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya kina mama kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) Dk. Lilian Mnabwiru, amesema kwa sababu utafiti huo ni wa kwanza kufanyika ni lazima ufanyike mwingine kama huo ili kuthibitisha matokeo hayo.

Alisema tafiti za aina hiyo ndizo zimekuwa zikisaidia kupatikana kwa majawabu ya magonjwa mbalimbali duniani katika jamii.

“Ni kweli kuna matatizo mengi na hilo linawezekana kinachotakiwa zifanyike tafiti nyingi hata sisi wataalamu wa hapa Tanzania tujikite kufanya tafiti nyingine kuona kama ni kweli hiki kilichoelezwa na hawa waliofanya utafiti huo,” alisema Dk. Lilian.

Kwa upande wake Dk. Salim  Maumba alisema upo uhusiano mkubwa kati ya mama mjamzito mwenye msongo wa mawazo na mtoto aliyepo tumboni, kwa sababu mama asipokuwa katika hali nzuri hata mtoto hawezi kuwa katika hali nzuri.

“Lakini siwezi kusema moja kwa moja mtoto anayezaliwa na mama aliyekuwa na msongo wakati wa ujamzito anaweza kuzaliwa na upungufu wa nguvu za kiume” alisema Dk. Maumba.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles