31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wajawazito 59 wapoteza uhai mkoani Mbeya

NA ELIUD NGONDO, MBEYA

ZAIDI ya vifo 59 vya mama wajawazito mkoani Mbeya, vimeripotiwa kutokea kuanzia Januari hadi Oktoba, mwaka huu kutokana na sababu mbalimbali.

Hayo yalisemwa jana na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Dk. Conrad Milinga, wakati wa mkutano wa wadau mbalimbali wa afya, wakati wa uzinduzi wa mradi wa kuhamasisha uwajibikaji wa jamii katika kuboresha afya ya mama na mtoto kwa mikoa ya Mbeya na Njombe.

Alisema takwimu za kitaifa zinaonyesha kuna vifo 556 vya wajawazito kwa kila vizazi hai 100,000 na ambavyo vimeripotiwa kutokea hali iliyosababisha Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan,  Novemba 6, mwaka huu kuzindua mpango wa jiongeze tuwavushe.

Alisema kuanzishwa mradi huo, kumekuja kuchangia jitihada za Serikali ambazo zimeshaanza kuchukuliwa kuhakikisha akina mama wajawazito wanakuwa salama wanapojifungua pamoja na watoto.

“Takwimu hizi ni kubwa na ndiyo maana wenzetu wameamua kutusaidia kupambana nalo kwa kuzindua mradi huu ambao utaisaidia jamii kuelewa namna ya kumsaidia  mama na mwana,” alisema Milinga.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Uzazi na Malezi Bora (Umati), Dk. Lugano Daimon, alisema mradi huo unafadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (Unicef), ambapo utakuwa ukitekelezwa kwa kutumia simu kuwahamasisha akina mama waweze kujifungua salama.

Alisema ni asilimia 63 ya akina mama wajawazito wanaopata huduma za kitaalamu wakati wa kujifungua hali ambayo bado inahitajika nguvu zaidi ili kuhakikisha vifo hivyo vinapungua.

Alisema pamoja na viashiria vya matumizi ya njia za uzazi wa mpango, bado kumekuwepo na tatizo hilo kwa kiwango cha asilimia 37 jambo ambalo linatakiwa kuendelea kupambana nalo ili akina mama hao waweze kujifungua salama na watoto wawe salama.

Dk. Daimon, alisema malengo ya mradi huo ni kuleta uwajibikaji wa wadau mbalimbali katika utoaji wa huduma bora ambazo zinalenga akina mama wanaohudhuria kliniki na wale wanaohudhuria wakati wakujifungua.

Naye Meneja Ukusanyaji Rasilimali Umati, Joseph Mwamwaja, alisema wameamua kutoa elimu kwa watu watakaohusika katika utekelezaji wa mradi wakati wa utoaji huduma za afya ili kuhakikisha watoto wanazaliwa wakiwa salama pamoja na mama wajawazito.

Alisema dira ya Umati ni kuona wananchi wa Tanzania wanakuwa na uhuru wa kupata huduma za afya bila matatizo yoyote.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles