27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wagonjwa wa saratani waongezeka hadi 6,500

Mwandishi Wetu – Lindi

WIZARA ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesema kutoka mwaka 2002 hadi sasa hivi kumekuwa na ongezeko kubwa la wagonjwa wa saratani kutoka 2,500 hadi 6,500 kutokana na mitindo tofauti ya maisha na mabadiliko ya sayansi na teknolojia.

Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa jana na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, akiwa katika ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma za afya na uhamasishaji kwa wakulima kujiunga na bima ya afya.

 “Kama Serikali, tumeshtushwa na ongezeko la wagonjwa wa saratani na magonjwa mengine yasiyo ya kuambukiza, mwaka 2002 wagonjwa wa saratani nchini walikuwa 1,500 hadi 2,000, lakini kwa takwimu za mwaka jana, wagonjwa wa saratani wameongezeka kutoka 2,500 hadi 6,500,” alisema Ummy.

Pia alisema Serikali imeona upo ulazima wa kuchukua hatua za makusudi katika kupambana na saratani ya mlango wa kizazi na magonjwa mengine yasiyo ya kuambukiza yakiwamo shinikizo la damu, magonjwa ya moyo na ugonjwa wa kisukari.

Alisema katika kila wagonjwa 100 wa saratani, 34 ni wa saratani ya mlango wa kizazi na 12 saratani ya matiti.

“Kibaya zaidi katika kila wagonjwa 100 wa saratani, 80 wanafika wakiwa wamechelewa na wengine ugonjwa ukiwa katika hatua ya tatu au ya nne, hivyo kupona kwao kunakuwa ni kugumu,” alisema.

Awali akisoma taarifa ya mkoa, Katibu Tawala Mkoa wa Lindi, Rehema Madenge, alisema wameanzisha utoaji wa chanjo ya kukinga saratani ya mlango wa kizazi (HPV) kwa wasichana wa umri wa miaka tisa hadi 14.

Alisema katika mwaka wa fedha wa 2017/2018 jumla ya mahudhurio 164,259 yalirekodiwa vituo vyote vya kutolea huduma za afya vya Serikali, binafsi na vile vya dini huku Hospitali ya Mkoa Sokoine ikirekodi mahudhurio 39,324 na kulipwa Sh 1,654,964,965 katika kipindi hicho.

 Rehema alisema mkoa umeendelea kuhudumia wanufaika wa Bima ya Afya ya Taifa (NHIF) kwa ufanisi mkubwa katika mwaka wa fedha wa 2017/2018.

Pia alisema ili kuwafikia wananchi wengi kupitia makundi mbalimbali, NHIF imekuja na mpango uitwao ushirika afya ambao wakulima wanaungana katika vyama vyao vya mazao na kuweka mkakati wa kujiunga na bima ya afya kwa utaratibu wa ushirika wao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles