24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

WAGONJWA WA FIGO MUHIMBILI ‘WAMLILIA’ RAIS MAGUFULI

NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM


WAGONJWA wa figo ambao wanasubiri huduma ya upandikizaji katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), wanatamani kuonana na Rais, Dk. John Magufuli, ili wamfikishie kilio chao kuhusu huduma hiyo.

Wakizungumza na MTANZANIA Jumamosi jana kwa sharti la majina yao kutotajwa gazetini, walisema licha ya kuwa tayari wamepata wachangiaji figo (donors) ili wafanyiwe upasuaji huo, wanashangaa hawapandikizwi.

Wamesema hata wanapoomba kwenda kutibiwa nje ya nchi huelezwa kwamba rufaa zimesitishwa na serikali, hivyo kutokana na hali hiyo wanaendelea kufanyiwa huduma ya kuchuja damu (dialysis) pekee hospitalini hapo.

“Mimi nina miaka miwili tangu nimeanza huduma ya dialysis, kila wiki nafanyiwa mara tatu, huwa nakuja Jumanne, Alhamisi na Jumamosi, kila ninapokuja ninalipia Sh 300,000, hivyo kwa wiki ninalipia Sh 900,000 kwa huduma hii pekee.

“Hapo sijajumlisha gharama nyingine, ikiwamo usafiri na dawa mbalimbali ambazo huwa tunatakiwa kutumia kama vile dawa ya kuongeza damu ambayo huwa ni sindano moja inayogharimu kati ya Sh 35,000 hadi 40,000 na kila ninapokuja huwa nachomwa.

“Bado kuna gharama za sindano nyingine ambayo huwa nachomwa ili kulainisha damu inapopita kule kwenye mashine isigande, hiyo huwa ni Sh 10,000 na inanunuliwa kila ninapokuja kliniki,” alisema mmoja wa wagonjwa wanaolalamika.

Alisema ikiwa atajumlisha na gharama nyinginezo pamoja na nauli yake na ya ndugu ambaye humsindikiza kliniki kila anapohudhuria, inaweza kuwa zaidi ya Sh milioni 100 kwa mwaka.

“Maisha yetu wengi ni magumu, nimelazimika kufunga biashara zangu huko Tanga kwa kuwa ninajiuguza huku Dar es Salaam, mke wangu ndiye aliyenisaidia kupata bima ya afya, najiuliza kama nisingekuwa nayo ingekuwaje,” alihoji mgonjwa huyo.

Alisema kutokana na changamoto hiyo, watoto wake wamekuwa wakihudhuria masomo kwa tabu na kusisitiza kwamba maisha yake kiujumla yametikiswa.

“Hapa (MNH) naona huduma zimesimama na hakuna tunachoelezwa, nashuhudia wengine wakipoteza maisha huku wakiwa tayari wamepata wachangiaji…tunazidi kuchoka, tunaomba Rais Magufuli asikie kilio chetu, tumewaeleza wasaidizi wake mara nyingi lakini nadhani hawafikishi kwake, tunaomba atusikie,” alisema.

Kutokana na malalamiko hayo, MTANZANIA Jumamosi lilimtafuta Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Faustine Ndugulile, ambaye alisema si kweli kwamba serikali imesitisha rufaa za wagonjwa nje ya nchi, wakiwamo wanaohitaji huduma ya upandikizaji figo.

 

Inaendelea………………… Jipatie nakala yako ya gazeti la MTANZANIA

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles