25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Wafugaji wamtisha Rais Kikwete

wafugajiNa Debora Sanja, Dodoma

WAFUGAJI wa Kanda ya Magharibi, wanakusudia kufanya maandamano kwenda Ikulu kwa ajili ya kudai haki yao iwapo Rais Jakaya Kikwete hataitoa kwa umma ripoti ya uchunguzi wa Operesheni Tokomeza.

Wamesema katika kuidai ripoti hiyo ya Tume ya Kijaji, pia watafunga minada yote ya mifugo ya Kanda ya Magharibi inayoundwa na mikoa ya Kigoma, Tabora, Katavi na Rukwa.

Kusudio hilo la kufanya maandamano lilitangazwa jana mjini Dodoma mbele ya waandishi wa habari na Katibu wa Chama cha Wafugaji wa Kanda ya Magharibi, Joseph Paroko.
“Ikifika Julai 30, Rais hajaweka hadharani taarifa ya Operesheni Tokomeza, wafugaji wa Kanda ya Magharibi tutafanya maandamano makubwa kwenda Ikulu kadai haki yetu,” alisema Paroko.

Alisema wafugaji wanataka taarifa hiyo iwekwe hadharani kwa sababu hadi sasa waathirika wa Operesheni Tokomeza hawajui hatima yao na pia wanaishi maisha magumu.

“Kwa mfano katika Kijiji cha Lumba, Wilaya ya Kaliua mkoani Tabora, ng’ombe 2,537 walipigwa mnada kwa kutumia jina la Operesheni Tokomeza.

“Rais aliagiza operesheni hiyo isake majangili lakini badala yake askari walikwenda hifadhi za misitu na kuwabambikizia kesi wafugaji,” alisema Paroko.

Alisema katika operesheni hiyo, baadhi ya wafugaji walitapeliwa ng’ombe na wengine waliuawa huku wakiwepo waliopata ulemavu wa kudumu kwa kupigwa risasi na askari lakini hadi sasa hawajui hatima yao.

Sambamba na hilo, Poroko alisema wafugaji wanataka Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro
Nyalandu, apeleke bungeni taarifa ya mapori ya hifadhi yaliyokosa sifa ya kuwa mapori ya akiba.

Alisema lengo la kuidai taarifa hiyo ni kulitaka Bunge litengue sheria ya mapori hayo kuendelea kuwa hifadhi na badala yake wapewe wafugaji kwa ajili ya kulishia mifugo yao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles