Na JONAS MUSHI-DAR ES SALAAM
MBUNGE wa Ubungo, Saed Kubenea (Chadema), amesema wafanyabiashara wote wadogo wa Manzese Midizini watahamishiwa katika Soko la Simu 2000 ili kuruhusu eneo hilo kujengwa kisasa.
Hayo aliyasema mwishoni mwa wiki wakati akifanya ziara jimboni kwake ambapo alitembela Kituo cha Simu 2000 kujionea maendeleo na chanagamoto zinazowakabili wafanyabiashara na uongozi wa kituo hicho.
“Tunataka ile Manzese iwe kama Dubai kwa kuipanga vizuri kuanzia mitaa na barabara zake ikiwemo kuwaondoa wamachinga wote waje Simu 2000 ambayo tunawatengenezea soko la kisasa,” alisema Kubenea.
Naye Meneja wa Kituo hicho, Elichilia Hamis, alisema changamoto iliyopo ni kuondoka kwa wafanyabiashara na kuacha vizimba zaidi ya 90 vikiwa wazi baada ya Rais John Magufuli kuruhusu biashara za mitaani.
Alisema changamoto nyingine ni kupungua kwa wateja wa soko na mapato ya kituo cha mabasi baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi kavu na Majini (Sumatra) kubadilisha ruti ya daladala zinazotoka Kibaha kuishia Mbezi badala ya kituoni hapo.
Akielezea mipango ya kuboresha soko hilo alisema litajengwa kisasa na kugawanywa katika sehemu nne ikiwemo sehemu ya matunda, mbogamboga na maduka.