KULWA MZEE, DAR ES SALAAM
Mahakimu, mawakili wa Serikali na binafsi, askari Magereza, Polisi, waandishi wa habari na watumishi wengine wa mahakama wamepatiwa mafunzo ya kujikinga na mambukizi ya virusi vya corona.
Wadau hao wamepatiwa mafunzo hayo asubuhi ya leo Jumatano Machi 25, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ambapo waliingia kwa makundi ili darasa liwe na watu wachache.
Akitoa mafunzo hayo, Sophia Ntomola kutoka Idara ya Afya Manispaa ya Ilala amesema wanatoa mafunzo sekta ya afya na kwa wananchi ili watoe taarifa sahihi.
“Taharuki iko sana mitaani, tukifanya kazi kwa taharuki tutashindwa hata kujikinga, tusifanye kazi kwa taharuki, tufuate njia za kujikinga.
“Tuendelee kuchukua tahadhari kwa jinsi tulivyojipanga, mwananchi akihisi afike kituo chochote cha afya kilichopo jirani atahifadhiwa na kupata msaada wa kwenda eneo sahihi lililopangwa kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi,”amesema Sophia.
Akijibu swali kuhusu bomba na sabuni za kunawia ikiwa aliyeambukizwa kagusa na mwingine akagusa hawezi kuambukizwa, alijibu kwamba inatakiwa kuwa na kifungio cha kufungua kwa kiwiko ili mtu asishike, lakini kwa kufunguliwa cha kawaida mtumiaji anaweza kuchukua maji akajinyunyizia ili kupunguza lakini inatakiwa kutumia kiwiko kufungua.