
NA MWALI IBRAHIM, DAR ES SALAAM
KIKOSI cha klabu ya Simba jana kimeanza mazoezi ya viungo ili kujiweka sawa wakati wakimsubiri kocha wao mkuu, Zdravko Logarusic, ambaye anatarajia kuwasili nchini leo na kuanza programu ya mazoezi rasmi kesho.
Wachezaji Ivo Mapunda, Uhuru Selemani, Awadh Juma Hassan Isihaka, William Lucian, Said Ndemla, Issa Rashid, Mohamed Hussein, Peter Manyika anayecheza nafasi ya kipa timu B walianza mazoezi chini ya kocha msaidizi, Selemani Matola katika gym iliyopo maeneno ya VETA Chang’ombe.
Mazoezi hayo yalidumu kwa saa mbili ambapo walianza na mazoezi ya kujenga stamina na baadaye wakaingia gym kutumia vifaa kwa ajili ya kuongeza pumzi pamoja na kujiweka fiti.
Rais wa klabu hiyo, Evance Aveva, awali alisema mazoezi hayo yangeanza rasmi jana wakiwa na kocha huyo, lakini imeshindikana kutokana na mipangilio ya usafiri.
Akizungumza mazoezini hapo kocha Matola alisema watafanya mazoezi hayo hadi programu ya Loga itakapoanza rasmi ambapo watakuwa wakifanya asubuhi mazoezi ya viungo na jioni uwanjani.
“Ratiba ya mazoezi itabadilika atakapowasili kocha, lakini kwa sasa ratiba itakuwa hii kwa ajili ya kuanza kujiimarisha,” alisema.
Kocha Loga anatarajia kuja na mikakati mipya ya kukinoa kikosi chake ambayo ameipanga akiwa nchini Croatia kwa mapumziko baada ya kumalizika kwa ligi msimu uliopita wa 2013/2014.