30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Wabunge ‘wamtimulia’ vumbi Waziri Mkuu, uchaguzi wanukia

LONDON, UINGEREZA

WABUNGE 344 wa Uingereza wamekataa mapendekezo ya makubaliano ya Brexit ya Waziri  Mkuu, Theresa May, juzi kwa mara ya tatu na kuashiria uwezekano wa kujiondoa mapema katika Jumuiya ya Ulaya, ikiwa ni ishara ya kutimuliwa vumbi ambalo linamchafua waziri huyo na huenda ikamlazimu kuitisha uchaguzi mkuu wa tatu nchini humo katika kipindi chake. 

Uamuzi wa kuukataa mpango uliofupishwa kidogo wa makubaliano ya  kujitoa katika Jumuiya hiyo kati ya Waziri May na Umoja wa Ulaya imeliacha suala la kujitoa kutoka  Umoja huo katika hali ya sintofahamu  kwa sasa, lini na ama hata iwapo  Uingereza itajitoa na kulitumbukiza suala hilo la mzozo wa Brexit lililodumu kwa muda wa miaka mitatu sasa katika kiwango kikubwa cha kutoeleweka linaelekea wapi.

Kwa mujibu wa gazeti la Daily Mail, Waziri Mkuu, Theresa May aliungwa mkono na wabunge 286, ambao hawakufua dafu mbele ya wenzao 344 ambao wamekataa mapendekezo ya Waziri Mkuu huyo, hivyo kulilazimu taifa hili kuharakisha mchakato wa kujiondoa kwenye Jumuiya ya Ulaya.

Nalo gazeti la Telegraphy limeripoti kuwa, kwa matokeo hayo pia yanaashiria kuwa Waziri May anapaswa  kujiuzulu mara moja baada ya kufanya  majadiliano ya muda ya kuongeza  uanachama wa muda wa Uingereza  katika Umoja wa Ulaya kushindikana.

“Hapaswi kuona au kuambiwa, kwamba  wakati anaweza kukutana na Umoja wa  Ulaya kujadili kurefushwa kwa muda wa kujiondoa kwenye Jumuiya ya Ulaya, ni  kitu cha kawaida kwamba ndio amefika  mwisho. Ni lazima ajiondoe, kwa ajili ya  Brexit, kwa chama chake na  demokrasia yenyewe,” ilisema tahariri ya gazeti la Telegraphy.

Aidha, gazeti hilo linalopendelewa na wanachama wa chama cha May cha Conservative na kuunga mkono juhudi za chama hicho katika siasa za Uingereza.

Hata hivyo, uwezekano wa kuwa na  Waziri Mkuu mpya kuongoza awamu  ijayo ya majadiliano ya Brexit ilikuwa  haitoshi kuweza kuwavutia wabunge  wa nchi hiyo katika zoezi la upigaji kura, baadhi yao wakihofia makubaliano yake yanaiacha Uingereza ikifungwa katika  Umoja wa Ulaya iwapo mazungumzo ya  hapo baadaye ya biashara yatavunjika.

Vyombo vya habari nchini Uingereza vimechambua kura hiyo kama hatua ya kuelekea kung’olewa madarakani kwa Waziri Theresa May au kuitisha uchaguzi mwingine. May, ambaye  amenusurika katika changamoto ya kumtoa  madarakani Desemba mwaka jana, amedokeza bungeni hapo juzi kwamba  angehitaji kuitisha uchaguzi mkuu wa  taifa kuweza kupata wingi kwa ajili ya  kupitisha sheria ya Brexit.

“Uwezekano wa May kuitisha uchaguzi na kuongoza  kundi la  wabunge  wa chama chake cha  Conservative kupata wabunge  wengi  watakaofikia theluthi ya wabunge  wote  bungeni, ni vigumu,” limesema gazeti moja.

Nchini Uingereza, vyombo vya habari vimepambwa na maoni ya kumtaka Theresa May kujiuzulu wadhifa wake kwakuwa ameshindwa kutafuta ufumbuzi wa Brexit.

Kwa upande wake, gazeti la Daily Mail ambalo linaunga mkono Brexit limeeleza uamuzi  wa bunge kupiga  kura dhidi ya mipango ya Theresa May  kuwa ni ‘usaliti’.

Kutokana na kura hiyo, Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya, Donald Tusk, ameitisha kikao cha baraza hilo ifikapo Aprili 10 mwaka huu, kujadili hali ya mambo ya mpango wa Uingereza kujitoa.

Viongozi kadhaa wa Ulaya wamesema  kuna nafasi halisi kwamba Uingereza  sasa itajiondoa bila kupata makubaliano ya kibiashara, hali ambayo  makampuni yanahofia itasababisha  mtafaruku kwa uchumi huo wa tano  mkubwa duniani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles