33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

‘Wabunge hudhurieni vikao kwenye halmashauri’

majaliwaSERIKALI imesema ni wajibu wa wabunge wote wenye majimbo na wale wa viti maalumu kuhudhuria vikao vya mabaraza ya madiwani kwenye halmashauri zao.
Kauli hiyo ilitolewa bungeni jana na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Kassim Majaliwa, wakati akijibu swali la Mbunge wa Meatu, Meshack Opulukwa (Chadema).
Katika swali lake, Opulukwa alitaka kujua kauli ya Serikali kuhusu baadhi ya wakurugenzi wa halmashauri kuwazuia wabunge kuhudhuria baadhi ya vikao vya halmashauri kwa madai kwamba hawajapangiwa kuhudhuria vikao hivyo.
Majaliwa alisema katika ngazi za halmashauri za wilaya vipo vikao vya aina mbili ambavyo ni Mkutano wa Halmashauri na Kamati za Kudumu za Halmashauri.
“Kwa mujibu wa kifungu cha 35(1)(c) cha Sheria ya Serikali za Mitaa pamoja na kanuni ya 6(I)(II) ya kanuni za kudumu za halmashauri za wilaya kwa mwaka 2013, zinaelekeza kuwa Mbunge atakuwa ni Mjumbe wa Mkutano wa Halmashauri, pia atakuwa ni mjumbe wa kamati zote za kudumu katika halmashauri husika.
“Kwa mujibu wa sheria na kanuni hizi, mbunge anastahili kuhudhuria vikao vyote, vikiwemo vikao vya Baraza la Madiwani, lakini pia mbunge ana haki ya kuhudhuria vikao vya kamati zote za madiwani zinapokutana kwa kuwa na yeye ni mjumbe kisheria,” alisema Majaliwa.
Alisema kwa mantiki hiyo, mbunge hapaswi kuzuiliwa kuhudhuria katika vikao vya halmashauri kwa sababu yeye ni mjumbe kwa kuzingatia sheria na kanuni za Mamlaka ya Serikali za Mitaa.
“Nazikumbusha halmashauri kuhakikisha wakati wote zinazingatia sheria na kanuni katika kuendesha vikao vya halmashauri ili kuepuka migogoro isiyokuwa ya lazima,” alisema Majaliwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles