26.9 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Waangalizi wa Demokrasia Endelevu Afrika watoa tathimini ya uchaguzi

NA ASHA BANI-DAR ES SALAAM

WAANGALIZI wa kimataifa wa Taasisi ya Uchaguzi na Demokrasia Endelevu Afrika (EISA),wamesema licha uchaguzi kufanyika kwa amani  na utulivu lakini kulikuwapo na dosari ndogo ndogo zilizojitokeza.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari kiongozi Mkuu wa timu ya waangalizi wa uchaguzi wa EISA, Pansy Tlakula, alisema  licha ya shughuli na taratibu nyingine za uchaguzi kwenda sawa na kwa weledi, lakini timu hiyo imebaini kasoro kadhaa za uchaguzi ikiwamo baadhi ya wagombea wa uchaguzi kuwekwa ndani  kwa makosa mbalimbali.

Alisema kila mtu ana wajibu wa kuheshimu sheria za nchi na ni muhimu pia, kwa taifa kujua kuwa zipo kanuni za kisheria zinazotakiwa kufuatwa katika mwenendo unaojenga imani katika mfumo wa uchaguzi.

Pia  timu ya waangalizi hao ilibaini  kasoro katika upatikanajii wa taarifa ikiwamo kufungiwa kwa baadhi ya vyombo vya habari na kuzuiwa kwa haki za uhuru wa habari na mwenendo bora wa uhuru wa kupata taarifa.

Alisema kasoro nyingine ni matumizi ya mabomu ya machozi katika maeneo ya kijiji cha Kagangani Zanzibar, kuzuiwa kwa mikutano ya siasa, maandamano na uhuru wa kujieleza.

“Kasoro nyingine ni pamoja na idadi ndogo ya wanawake katika chaguzi za Tanzania na hivyo kuitaka Serikali kuhimiza utoaji wa fursa kwa wagombea wanawake kuingia majimboni,”alisema Tlakula.

Aliongeza kuwa  uwepo wa viti maalum kwa wabunge wanawake ni muhimu na umeongeza uwakilishi katika bunge hivyo ni vyema idadi hiyo ikaongezeka pia.

Timu ya waangalizi imepongeza uwepo wa karatasi maalum kwa wapiga kura wenye ulemavu wa macho (nukta nundu) uliowezesha uhuru na siri wakati wa upigaji kura.

“Tumeshuhudia, juhudi zinazofanywa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ya kufanya mikutano ya kila wiki na vyombo vya habari na wanahabari. Mikutano hiyo inatoa nafasi kwa vyombo vya habari na tasnia ya habari kujadiliana na kuelimishana kuhusu sheria na kanuni za habari,” Tlakula

Ujumbe wa EISA unajumuisha waangalizi 14 waliotoka katika asasi mbalimbali za kiraia na menejimenti za uchaguzi kutoka nchi mbalimbali za Afrika.

Waangalizi hao wametoka Uganda, Afrika Kusini, Zimbabwe, Rwanda na Malawi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles