30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

WAANDAJI KAGAME CUP MJITAFAKARI UPYA


Na JENNIFER ULLEMBO-DAR ES SALAAM

UKWELI michuano ya Kombe la Kagame 2018 haijaonyesha mvuto wowote, tofauti na ilivyokuwa miaka ya nyuma.

Hongera Azam FC kwa kufanikiwa kutetea taji hilo kwa mara ya pili mfululizo, pia pongezi zizifikie timu zote zilizoweza kushiriki michuano hiyo.

Michuano ya mwaka huu imefanyika kukamilisha ratiba na kupata mshindi tu, wala hakuna ushindani ulioweza kuonyeshwa na timu shiriki.

Kujiondoa kwa Yanga katika michuano hiyo ndiyo kumezidisha kupotea kwa mvuto zaidi, kuna haja waandaaji kujitafakari upya.

Mwanzo hadi mwisho wa michuano hiyo, mwitikio wa wadau na wapenda soka viwanjani umekuwa mdogo, ikilinganishwa na miaka iliyopita.

Michuano hiyo ambayo inaandaliwa na Baraza la Soka la Afrika Mashariki na Kati (Cecafa), inahitaji marekebisho na ubunifu mkubwa kurudisha hadhi yake ya zamani.

Marekebisho ya michuano hii yanapaswa kuanzia kwenye uongozi wa juu Cecafa hadi ngazi za nchini.

Miaka ya nyuma michuano hiyo ilikuwa  ikipendwa sana, idadi kubwa ya mashabiki walijitokeza uwanjani kushuhudia timu zao.

Lakini mwaka huu imekuwa tofauti kabisa, ushindani umekuwa mdogo kwa timu shiriki, hivyo ni vema wahusika wakajitafakari mapema.

Michuano hii imeanza kuonyesha dalili za kupoteza mwelekeo tangu ilipofanyika mara ya mwisho mwaka 2014.

Sababu iliyopelekea michuano hiyo kusimamishwa ghafla hadi leo haijulikani, kwa staili hii lazima hata timu ambazo zimekuwa zikishiriki mara kwa mara kukosa matumaini na waandaaji.

Kitendo cha michuano hiyo kusimama ndani ya miaka mitatu kimechangia kuishushia heshima na kuipotezea hadhi.

Ukweli unauma, lakini ni kheri ukasemwa ili kusaidia maboresho kufanyika, umefika wakati viongozi  wenye dhamana ya kusimamia michuano hii kujitafakari upya.

Hakuna haja ya kufurahi kupatikana kwa bingwa ikiwa michuano inarudisha nyuma maendeleo ya mpira wa miguu.

Hakuna mafanikio yasiyotokana na mabadiliko, hivyo lazima viongozi wa Cecafa mkubali kubadilika ili mjenge upya kurudisha hadhi na heshima ya michuano hii.  

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles