Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital
Viongozi wakuu wa Chadema wakiongozwa na Mwenyekiti, Tundu Lissu, na Katibu Mkuu, John Mnyika, wanadaiwa kupanga kumfukuza uanachama Lembrus Mchome, baada ya kada huyo kuhoji uteuzi wa viongozi wa sekretarieti na wajumbe wa Kamati Kuu.
Mbali na Lissu na Mnyika, pia Godbless Lema anatajwa kuunga mkono hatua hiyo, huku mpango kabambe wa kumvua Mchome uanachama na uenyekiti wa Chadema Wilaya ya Mwanga ukiwa tayari.
Hata hivyo, baadhi ya makada waandamizi wa Chadema wameapa kusimama na Mchome endapo atafukuzwa, wakidai kuwa hana kosa lolote. “Hatutakubali uonevu huu, tutamsapoti hata kama ataenda mahakamani,” amesema mmoja wa makada.
Mchome, kupitia barua yake kwa Mnyika iliyosambaa mtandaoni, alihoji uhalali wa uteuzi wa viongozi wa Kamati Kuu na sekretarieti bila akidi kutimia katika kikao cha Januari 22.
Mpasuko ndani ya Chadema unaendelea kukua, huku baadhi ya wanachama wakidai kuwa mgawanyiko kati ya makundi yanayomuunga mkono Lissu na Freeman Mbowe unazidi kuleta mtikisiko. Pia, msimamo wa “No Reforms, No Election” unaonekana kuzua sintofahamu kwa wanachama wengi.