26.9 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

VIWAVI JESHI WAVAMIA MASHAMBA MOROGORO

Na LILIAN JUSTICE- MOROGORO

WANANCHI katika vijiji vinne vilivyopo Kata ya Bwakila Chini, Wilaya ya Morogoro, viko hatarini kukumbwa na njaa baada ya mazao yao kuvamiwa na viwavi jeshi.

Uwepo wa wadudu hao ulielezwa juzi na baadhi ya wananchi hao walipokuwa wakizungumza na MTANZANIA.

Wananchi hao, Etros Munyi na Yassin Mnungu, walisema kama hatua za haraka hazitachukuliwa ili kukabiliana na wadudu hao, hali inaweza kuwa mbaya zaidi.

Walivitaja vijiji vilivyo katika hatari ya kukumbwa na njaa kuwa ni pamoja na Bwakila Chini, Dakawa, Bonye na Mbwade ambako mazao yameshaharibiwa na wadudu hao.

Kwa upande wake, Ofisa Kilimo na Ushirika wa Kijiji cha Bonye, Filimon Mbaga, alisema mashamba yaliyovamiwa na viwavi jeshi ni hekta 375 za mahindi.

Pia alisema mashamba ya mpunga ni hekta 178 na nyasi za malisho ni hekta 500 ambazo tayari zimeshaharibiwa.

“Pamoja na hali hiyo, bado dawa za kuulia wadudu hazijafika katika maeneo husika, lakini ninatoa wito kwa wananchi kuendelea kununua dawa hizo katika maduka ya pembejeo badala ya kuisubiri Serikali.

“Wananchi wasikae tu na kusubiri Serikali iwaletee hayo madawa na badala yake wakayanunue madukani kwani kama wataendelea kuisubiri Serikali wanaweza kuathirika zaidi.

“Wadudu hao waharibifu walianza kujitokeza mwezi Februari mwaka huu kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa, lakini wameanza kupungua kufuatia mvua nyingi zinazonyesha,” alisema Mbaga.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, Sudi Mpili, alisema tayari wameshatuma maofisa ugani kukabiliana na wadudu hao.

“Kuna wataalamu wameshatumwa huko ili kufanya tafiti juu ya wadudu hao,” alisema Mpili.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles