30.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Vituo viwili vya uchenjuaji madini vyafungwa kwa kutiririsha maji yenye sumu

Na Denis Sinkonde, Songwe 

HALMASHAURI ya Wilaya ya Songwe mkoani Songwe imeandika barua ya kusitisha huduma na ujenzi katika vituo viwili vinavyotumika kuchenjulia madini ya dhahabu (PLANT) kwa madai kuwa maji yenye sumu yanatililika kwenye makazi ya watu ikiwemo kwenye vyanzo vya maji.

Wilaya ya Songwe asilimia 80 ya mapato yake hutegemea uchimbaji wa madini, kilimo, ufugaji na uvuvi lakini imedaiwa kuwa wawekezaji wa kati na wachimbaji wadogo wengi wao hawazingatii sheria wakiharibu mazingira kwa kufunga makarasha kwenye maeneo ya vyanzo vya maji na hata kwenye makazi ya watu na kuzua hofu kwa wananchi.

Kikao Kikiendelea…

Agizo hilo la kuzifungia Plant hizo mbili zimekuja baada ya madiwani kupitia kikao chao cha kawaida cha robo ya tatu kilichofanyika mwishoni mwa wiki kuibua hoja ya kumtaka mtumishi aliyehusika kutoa kibali kwa wachimbaji hao kuruhusu kujenga kwenye vyanzo hivyo vya maji kutoa amelezo.

Diwani wa kata ya Mbuyuni, Nawal Patani, alisema alipata malalamiko kutoka kwa wananchi pamoja na viongozi wa kijiji kuhusu mchimbaji kujenga Plant ya uchenjuaji kwenye vyanzo vya maji ndipo alipomfuata mmiliki wa mradi huo katika eneo hilo kumuuliza ambapo alimjibu kuwa ameruhusiwa na viongozi wa wilaya akiwemo Afisa Mazingira wa Wilaya, Jeremia Kaulananga.

Amesema baada ya kujibiwa hivyo, alipeleka lalamiko hilo kwenye kikao cha baraza na baada ya kuliibua madiwani wakaja juu alipoulizwa Afisa mazingira alikana kutoa kibari na kwamba kijiji cha Iseche ndipo mradi ulipo jengwa na kuna wakazi zaidi ya 5,000 wanategemea maji kutoka chanzo cha kijiji cha Iseche na endapo Plant hiyo inaanza kazi maji yote yenye sumu yataenda kwenye chanzo hicho na wananchi watazurika na hata kupoteza maisha na kwamba aliomba ujenzi usitishwe.

Kaulananga alipoulizwa kuhusu ujenzi wa mradi huo kwenye chanzo cha maji, alisema yeye wala hafahamu nakwamba hajatoa kibali hivyo kunauwezekano aliyejenga hapo alivamia posipo kufika kwenye ofisi husika.

Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Abraham Sambira alikuagiza Mkurugenzi Mtendaji kuandika barua ya kusitisha ujenzi wa Planti hiyo ya Iseche inayomilikiwa na Merrykyad Kabika iliyojengwa kwenye chanzo cha maji na kusitisha matumizi ya Plant ya Mbangala inayomilikiwa na Fortery inayotililisha maji yenye sumu kwenye makazi ya watu na kuunda timu ya uchunguzi kumbaini kiongozi aliyetoa vibali vya ujenzi huo.

‘’Hivi inawezekanaje muwekezaji ajenge mradi utakao mwaga maji yenye sumu kwenye chanzo cha maji alafu afisa mazingira asijue? Timu ya uchunguzi itatupa majibu ndani ya siku 7, atakayebainika itakula kwake pia nakuagiza mkurugenzi simamisha ujenzi hadi uchunguzi ukamilike,’ amesema Sambira.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Abdulkadir Mfilinge, alisema ameyapokea maagizo hayo na kuahidi kuyafanyia kazi huku akitoa angalizo kwa watumishi wanaokiuka kanuni za utumishi akiahidi hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.

Ikumbukwe wilaya Songwe ni moja ya wilaya nchini inayokabiliwa na mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu kutokana na wananchi kunywamaji yasiyo salama, lakini Rais Samia Suluhu Hassan ametoa Sh Bilioni 6 kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maji, uharibifu kwenye vyanzo vya maji vinaweza kukwamisha miradi hiyo.

NJE YA KIKAO.

Evalisti Macho mkazi wa kijiji hicho amesema alipoona mwekezaji amevamia eneo hilo na kujenga mradi huo akiwa na wanakijiji wenzake walienda ofisi ya kijiji kuuliza na walipomfuata muwekezaji huyo alisema amemalizana na viongozi ngazi ya wilaya akiwemo afisa mazingira.

Gaudence Otto, Mwenyekiti wa kijiji hicho, alisema mwekezaji huyo alipokuja kununua eneo hilo yeye alikuwepo kama shahidi huku akidhani anataka kujenga nyumba ama kulima lakini akashangaa kuona matenki 17 ya uchenjuaji madini yakijengwa pasipo ofisi yake kujua.

Upande wake, Justa Chuki ambaye ni Afisa Mtendaji wa kijiji hicho alisema asilimia 90 ya wakazi wanategemea maji kutoka katika chanzo hicho, alishangaa kuona matenki hayo yanajengwa huku mashine za kusaga mawe zikianza kufanya kazi, alipomuuliza sababu ya kujenga katika chanzo cha maji alisema amemalizana na viongozi wa ngazi ya wilaya.

Nae, Mmiliki wa Mradi huo, Merrykyad Kabika alipofuatwa kwenye mradi huo hakuwepo na alipopigiwa simu iliita bila kupokelewa baada ya kufahamu kuwa wanahabari walioongozana na uongozi wa halmashauri wamefika kwenye mradi huo na kujionea jinsi uharibifu huo kwenye vyanzo vya maji.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles