27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Vitambulisho vya Taifa kutolewa upya

sefueNa Elizabeth Hombo, Dar es Salaam

MCHAKATO wa utoaji wa vitambulisho vya Taifa unatarajiwa kuanza upya, kutokana na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), kukiri kuwapo kwa upungufu katika vitambulisho vya sasa.

Katika taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari Dar es Salaam jana na Kitengo cha Mawasiliano na Hifadhi Hati, mamlaka hiyo inakiri kuwa vitambulisho vya Taifa vilivyogawiwa kwa wananchi kutokuwa na saini za wamiliki ni upungufu.

Taarifa hiyo ilisema kwa sasa NIDA inafanya jitihada za kurekebisha kanuni, taratibu na muundo wa vitambulisho hivyo ili kukidhi mahitaji ya wadau.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa, baada ya marekebisho hayo vitambusho hivyo sasa vitakuwa na saini mbili, ikiwamo ya mmiliki kwa upande wa mbele na saini ya Mkurugenzi Mkuu kwa upande wa nyuma.

Wakati mamlaka hiyo ikijiandaa kufanya marekebisho hayo, tayari wananchi wengi wamekwishagawiwa vitambulisho visivyokuwa na saini, huku ikiwataka wananchi wenye vitambulisho hivyo kusubiri maelekezo mengine.

“Mamlaka inakiri kwamba vitambulisho vya Taifa vilivyogawiwa havina saini pande zote. Tunafanya jitihada za kurekebisha kanuni, utaratibu na muundo wa vitambulisho ili kukidhi mahitaji ya wadau.

“Kuweka saini juu ya vitambulisho vya Taifa kunawezesha utambuzi na uthibitishaji wa taarifa za mmiliki wa kitambulisho cha Taifa ambao haulazimu kutumia alama za vidole.

“NIDA inawashukuru wadau wote kwa maoni yao hususani suala la kuweka saini juu ya vitambulisho vya Taifa ili kurahisisha utambuzi wa mmiliki wa kitambulisho na matumizi mengine ambayo tumeona ni budi kuyafanyia marekebisho,”ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa, NIDA itatatangaza tarehe rasmi ya kuanza kutolewa kwa vitambulisho vilivyofanyiwa maboresho na maelekezo kuhusu vile vilivyogawiwa ambavyo havina saini.

“Wadau wote wa NIDA ambao wana vifaa maalumu vya kusoma taarifa zilizomo kwenye kitambulisho (Card Readers) na ambao wameunganisha mifumo yao ule wa usajili na utambuzi wa watu wataendelea kutumia njia hizo kuthibitisha taarifa na utambuzi wa watu,”ilisema taarifa hiyo.

Gharama

NIDA ilitumia gharama ya zaidi ya Sh bilioni 179.6 kukamilisha mchakato wa uandaaji na utoaji wa vitambulisho vya Taifa, gharama ambayo ilizua mjadala mkubwa.

Kutokana na hali hiyo, Rais Dk. John Magufuli alimsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo, Dickson Maimu ili kupisha uchunguzi kutokana na fedha hizo kudaiwa kutumika vibaya katika kazi hiyo.

Hata hivyo haikuweza kufahamika mara moja iwapo mchakato wa utoaji wa vitambulisho hivyo utaanza upya, NIDA itatumia bajeti ipi katika kufanikisha maboresho hayo.

MTANZANIA ilifanya jitihada za kuwatafuta viongozi wa NIDA ili waweze kuzungumzia juu ya gharama mpya na mchakato mzima wa maboresho hayo, lakini hadi tunakwenda mtamboni juhudi hizo ziligonga mwamba.

Rais Magufuli

Januari 26, mwaka huu Rais Magufuli alitangaza kumsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa, Dickson Maimu, ili kupisha uchunguzi dhidi yake.

Maimu alisimamishwa pamoja na maofisa wengine wanne wa NIDA kwa tuhuma za ubadhirifu wa fedha za Serikali.

Maofisa hao ni Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano Joseph Makani, Ofisa Ugavi Mkuu Rahel Mapande, Mkurugenzi wa Sheria Sabrina Nyoni na Ofisa Usafirishaji George Ntalima.

Akitangaza uamuzi huo, Balozi Ombeni Sefue alisema taarifa zilizomfikia Rais zinaonesha kuwa NIDA hadi wakati huo ilikuwa imetumia Sh. bilioni 179.6 kiasi ambacho ni kikubwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles