WASHINGTON, MAREKANI
VIONGOZI wakuu wa Chama cha Republican nchini Marekani, wamemtaka mgombea wao wa urais, Donald Trump, ampishe mgombea wake mwenza, Mike Pence, kuwania kiti hicho.
Hatua hiyo imekuja kutokana na kuibuika kwa video anayosikika akiwadhalilisha wanawake.
Lakini Trump amesema kuwa hatajiondoa kutoka katika kinyang’anyiro cha kuwania kiti hicho, licha ya malalamiko kuhusu matamshi yake ya kuudhi kuwahusu wanawake aliyoyatoa mwaka 2005.
Zaidi ya wanasiasa 24 wa chama chake, sasa wamesema hadharani kuwa hawamuungi mkono bilionea huyo na wanataka badala yake, Pence achukue nafasi yake kuwania urais katika uchaguzi mkuu utakaofanyika mwezi ujao.
Pence na mke wa Trump, Melania, ni miongoni mwa waliolaani vikali matamshi hayo.