25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

VIJANA KUTUMIA KURA KUDHIBITI SILAHA MAREKANI

NEW YORK, MAREKANI


MAELFU ya vijana na wanaowaunga mkono wameandamana kote Marekani kudai udhibiti mkali wa silaha nchini hapa, wakiapa kutumia nguvu ya kura kutimiza lengo hilo.

Waliingia katika mitaa ya mji mkuu wa taifa hilo na miji mingine kama Boston, New York, Chicago, Houston, Minneapolis, Phoenix, Los Angeles na Oakland, California.

Idadi hiyo ya waandamanaji, ambayo ilikumbushia enzi za Vita vya Vietnam, iliwazoa wanaharakati, ambao kwa muda mrefu wamevunjwa moyo na mkwamo wa mjadala wa umiliki wa silaha na walizijumuisha sauti nyingi mpya za vijana.

Walihamasishwa na viongozi wapya kabisa: Wanafunzi walionusurika shambulio la shule mjini Parkland, Florida ambalo liligharimu maisha ya watu 17 Februari 4 mwaka huu.

“Ukisikiliza kwa karibu zaidi, unaweza kusikia watu walioko madarakani wakitetemeka,” alisema mmoja wa walionusurika shambulio hilo, David Hogg mbele ya umati wa waandamanaji waliofurika mtaa wa Pennsylvania mita chache kutoka majengo ya Bunge na karibu na Ikulu ya Marekani, White House.

“Tunalipeleka hili kwenye uchaguzi, kwa kila jimbo na kila mji. Tutahakikisha watu bora zaidi wanaingia na kugombea katika uchaguzi wetu, si kama wanasiasa lakini bali Wamarekani wanaoguswa na wimbi la ukatili wa silaha moto.”

Baadhi ya sauti za vijana zilikuwa za wadogo kiumri akiwamo Yolanda Renee King (9), mjukuu wa mwanaharakati wa haki za kiraia, marehemu Martin Luther King Jr.

Mjukuu huyo wa King alinukuu kutoka maneno maarufu ya kiongozi huyo wa haki za kiraia, akisema: “Nina ndoto kwamba inatosha. Kwamba huu unapaswa kuwa ulimwengu ulio huru na silaha.”

Chama cha Wamiliki wa bunduki kilibakia kimya kwenye ukurasa wake wa Twitter wakati maandamano hayo yakianza, ikilinganishwa na Machi 14, kilipochapisha picha ya bunduki na ujumbe usemao, ‘nitadhibiti bunduki zangu mwenyewe, ahsante.’

Rais Donald Trump alikuwa jimboni Florida kwa mapumziko ya mwishoni mwa wiki na pia hakuandika chochote kwenye twitter.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles