31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

VIGOGO WA SOKA ULAYA KUONESHANA UBABE WIKI HII

BADI MCHOMOLO NA MITANDAO


MICHUANO ya Ligi ya Mabingwa barani Ulaya inatarajia kuendelea wiki hii huku miamba ya soka barani humo ikitarajia kuoneshana ubabe wao.

Hatua hiyo ya robo fainali itazikutanisha timu nane katika michezo ya awali ambayo itapigwa Jumanne na Jumatano ya wiki hii.

Mtanzania SPOTIKIKI leo hii inakuletea uchambuzi katika mzunguko wa awali wa michezo hiyo ya robo fainali.

Juventus vs Barcelona

Huu ni miongoni mwa mchezo ambao unatarajia kuteka hisia za watu wengi wiki hii kutokana na ubora wa timu hizo katika michuano mbalimbali.

Mchezo huo utaanzia nchini Italia ambapo Juventus watakuwa kwenye uwanja wa nyumbani na kuwakaribisha mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu nchini Hispania.

Barcelona ilionesha kiwango cha hali ya juu katika mchezo wa hatua ya 16 bora dhidi ya PSG ya nchini Ufaransa, ambapo Barca iliweza kushinda mabao 6-1 kwenye Uwanja wa Nou Camp, wakati mchezo wa kwanza ambao ulipigwa kwenye Uwanja wa PSG, Barcelona walikubali kichapo cha mabao 4-0.

Wachache ambao waliamini kuwa Barcelona wangeweza kusonga mbele hatua ya robo fainali kutokana na idadi kubwa ya mabao ambayo walifungwa ugenini, lakini waliweza kugeuza matokeo na kuwafanya wasonge mbele.

Kesho Barcelona watakuwa wageni wa Juventus kwenye uwanja ambao unachukua idadi ya mashabiki 41,507.

Juventus wamekuwa watumwa kwa Barcelona, lakini mchezaji wa zamani wa klabu hiyo ya Juventus, Andrea Pirlo, amedai klabu hiyo ina nafasi kubwa ya kufuzu na kutwaa ubingwa msimu huu dhidi ya Barcelona.

Timu hizo zimekutana mara saba katika michuano hiyo mikubwa na Juventus imeshinda mara mbili na kupata mabao saba huku Barcelona ikishinda mara tatu na kupata mabao 10 wakitoka sare mbili, hivyo nani ataweza kutamba kesho?

Michezo sita ya mwisho ambayo Juventus wamecheza msimu huu imefanikiwa kushinda mitatu na kutoa sare miwili huku ikifungwa mmoja, wakati huo Barcelona ikishinda michezo mitano na kupoteza mchezo mmoja.

Dortmund vs Monaco

Katika mchezo huo mwingine wa kesho Dortmund watakuwa kwenye uwanja wa nyumbani na kuwakaribisha wapinzani wao Monaco kutoka nchini Ufaransa, katika mchezo huo, Dortmund wanapewa nafasi ya kuutumia vizuri uwanja wa nyumbani.

Dortmund iliweza kuingia hatua hiyo baada ya kuitoa Benfica, wakati huo Monaco iliweza kuitoa Manchester City.

Hata hivyo, Monaco wamekuwa na ushindani mkubwa msimu huu hivyo chochote kinaweza kutokea katika mchezo huo wa kesho bila kujali watakuwa kwenye uwanja wa ugenini.

Atletico Madrid vs Leicester City

Keshokutwa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu nchini England watakuwa kwenye uwanja wa nyumbani na kuwakaribisha watoto wa Diego Simeone, Atletico Madrid.

Leicester wameweza kupambana kwa mara yao ya kwanza kufika hatua hiyo ya robo fainali, lakini wengi wanaamini kuwa hatua hiyo ndiyo safari yao ya mwisho kutokana na ubora wa wapinzani wao.

Atletico Madrid ina wachezaji wenye uwezo mkubwa kama vile Antoine Griezmann, Fernand Torres katika safu ya ushambuliaji huku Leicester City wakiwa na nyota wao kama vile Jamier Vardy, Riyad Mahrez pamoja na wengine wengi.

Leicester City hawana uzoefu mkubwa wa michuano hiyo kama ilivyo kwa Atletico, lakini wanaamini kuwa chochote kinaweza kutokea.

Bayern Munich vs Real Madrid

Huu ni mchezo mwingine ambao utafunga wiki hii na kuacha simulizi kubwa kwa wadau na mashabiki wa soka duniani.

Madrid ambao ni mabingwa watetezi wa kombe hilo wataanzia ugenini dhidi ya wapinzani wao wababe wa nchini Ujerumani katika Ligi ya Bundesliga, Bayern Munich.

Bayern Munich kikosi cha kocha wa zamani wa Madrid, Carlos Ancelotti, kimeweka wazi kuwa kitahakikisha kinawasambaratisha wapinzani wao.

Bayern Munich wanaonesha kuwa wapo katika ubora wa hali ya juu msimu huu huku nafasi hiyo wakiingia baada ya kuichapa Arsenal jumla ya mabao 10-2, mchezo wa kwanza wakiwafunga mabao 5-1 na unaofuata wakifanya hivyo hivyo.

Madrid wao waliingia robo fainali baada ya kuifunga Napoli jumla ya mabao 6-2, ikiwa mchezo wa kwanza wakiwafunga mabao 3-1 sawa na mchezo uliofuata.

Nani atatamba katika mchezo wa wiki hii kabla ya marudiano wiki inayofuata?

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles