23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

VAT kupunguza watalii nchini kwabishaniwa

lion-in-tree

Na WINFRIDA NGONYANI-DAR ES SALAAM.

SEKTA ya utalii ndio sekta ya kwanza katika kuchangia fedha za kigeni kwenye uchumi wa taifa letu ukilinganisha na sekta nyingine .

Utalii ni miongoni mwa sekta muhimu sana katika kuchangia pato la taifa.

Sekta hii kwa mwaka 2015 imeweza kuchangia katika uchumi wa taifa dola za Kimarekani bilioni 2.23.

Pia, sekta ya utalii imekuwa ikitoa ajira kwa wengi nchini, na inalitangaza taifa letu kimataifa,

licha ya kuwa sekta hii ni muhimu na imekuwa ikilingizia taifa fedha nyingi za kigeni, lakini  haijatazamwa kwa kina kwani inauwezo wa kuingizia taifa mapato mengi zaidi.

Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Utalii Nchini (TCT), Mohamed Abdulkadir, anasema sekta ya utalii inaweza kuliingizia taifa mapato mengi zaidi sio tu kwa kupitia makusanyo ya kodi, bali pia katika nyanja zingine zinazoendana na utalii.

Bajeti ya mwaka 2016/17 imepitisha tozo ya kodi ya ongezeko la thamani VAT kwa asilimia 18 kwenye huduma za utalii.

Hususan katika shughuli za kuongoza watalii, kusafirisha watalii, utalii wa majini, kuangalia wanyama na ndege wa porini, kupiga picha, kutembelea hifadhi na usafirishaji wao.

Baada ya bunge kupitisha sheria hiyo mpya kuanzia Julai mosi mwaka huu, Serikali imeanza kutoza kodi ya VAT kwenye shughuli za utalii.

Hutua hiyo ya serikali kwa maelezo ya Abdulkadir alionesha wasiwasi wake wa kupungua kwa idadi ya utalii nchini hata kabla sheria haijapitishwa wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake hivi karibuni. Hivyo kuzidi kuonesha kuwa hisia inatawala zaidi kuliko ukweli.

Anasema Tanzania itapoteza idadi kubwa ya watalii wanaokuja nchini kwani biashara ya utalii ina ushindani mkubwa na mabadiliko yoyote ya bei huleta ukakasi au huvuruga mipanago kwani huwa ni ya muda mrefu.

Anaongeza kuwa, Serikali hapo awali ilikwishaamua kutotoza kodi hii katika sekta ya utalii kwa sababu kadhaa na sababu hizo hadi sasa bado hazijatatuliwa.

Abdulkadir anaeleza ilikuwa ni kwamba sekta hii bado changa na kwa hivyo inahitaji kulelewa kwani ina changamoto nyingi ambazo zinahitaji kutatuliwa kwanza.

Anasema, kutoza kodi hii inaifanya Tanzania kupoteza nafasi yake ya ushindani wa kibiashara.

Kodi ya ongezeko la thamani itaongeza gharama ya watalii kuja Tanzania kwa zaidi ya asilimia 18,” anasema Abdulkadir.

Anaeleza kuwa, tayari nchi mshindani mkuu wetu katika biashara hii ambayo ni nchi ya Kenya imeondoa kodi ya ongezeko la thamani kwenye utalii iliyokuwa inatoza kwa asilimia 16 ili kuichuuza Tanzania na hivyo ni kucheza shere kwa nchi wakati walikubaliana wafanye hivyo.

Uchezaji huu wa rafu unaifanya nchi hiyo kuwa ionekane kuwa  ni rahisi.

“Hii ina maana watakua katika nafasi kubwa ya kiushindani na sisi na hivyo kama sisi tutaweka kodi hii kwa asilimia 18 basi tunaweza kupoteza idadi kubwa ya watalii ambao wangekuja nchini kwetu,”anasema Mwenyekiti huyo.

Anafafanua zaidi kuwa, tayari Kenya ambayo ilitumiwa kama mfano wakati wa hotuba ya Waziri wa Fedha Dk Philip Mipango, aliyeitoa katika bunge la bajeti lililomalizika, wamekwishaondoa kodi hii baada ya kuona madhara yake kwenye utali.

Hili ni fundisho kwetu kutojaribu kufanya makosa hayo ambayo Kenya waliyafanya.

Katika hotuba yake aliyoitoa katika bunge la bajeti la mwaka 2016/17, Dk Mipango alisema, miongoni mwa sababu za kuongeza kodi hii ni kuwa Tanzania haina budi kuongeza kodi ya VAT kwenye shughuli za utalii kwa kuwa wenzetu Afrika ya Kusini wanatoza kodi hiyo na watalii wanaendelea kuingia nchini humo.

Abdukadir anaeleza kuwa, Afrika Kusini si mfano wa kutumia kulinganisha na sekta ya utalii wa nchi yetu kwa kuwa sekta ya utalii nchini Afrika Kusini imekua kwa kiasi kikubwa na aina ya utalii wa nchi hiyo haifanani na Tanzania.

“Hata hivyo, wakati Afrika ya kusini ikiwa na watalii zaidi ya milioni 10 na miundo mbinu bora sana ya usafiri wa anga na huduma za hoteli hutoza tozo kiwango cha asilimia 14 kodi.

Uchumi wetu wa utalii unahitaji kukua zaidi ya mara kumi ndivyo tuweze kujilinganisha na Afrika ya Kusini,”anafafanua zaidi Abdulkadir.

Abdulkadir anasema, biashara hii ya utalii tunaifanya lakini kuna ushindani mkubwa kutoka nchi kama vile Kenya, Afrika Kusini, Botswana na Namibia ambazo bidhaa zake zinalingana na zetu.

Anasema, nchini kuna utitiri wa kodi kwenye shughuli za utalii kama vile kodi ya kuingia kwenye hifadhi za taifa, ushuru wa kwenye hoteli, pamoja na hii kodi ya VAT ya asilimia 18.

Anaeleza zaidi kuwa viongozi wetu wanapaswa kuelewa kuwa biashara kwenye sekta ya utalii inafanywa kwa msimu wa utalii na hufanywa na mawakala nje ya nchi na hivyo kuweka ongezeko la kodi bila kuzingatia muundo wa biashara hii ni kupunguza idadi ya watalii nchini.

Anashauri badala ya kufikiri zaidi kuingiza kipato kutokana na makusanyo ya kodi kwenye utalii tunapaswa kufikiri faida nyingine zinazoweza kupatikana kwenye utalii kama vile kutoa ajira kwa vijana na kuitangaza taifa kimataifa.

 

Anasema kuwa, taifa linaweza kufaidika na sekta ya utalii kwa kuhakikisha kuwa tunakuwa na ndege za taifa, kuboresha usafiri wa anga ambao utasaidia kuongeza pato la taifa kwa kuwa watalii watatumia usafiri wa taifa.Aidha, Abdulkadir anasema kwenye sekta ya utalii, nyanja ambayo ilikuwa ikiingiza fedha nyingi ambayo sasa hivi imekufa ni utalii wa uwindaji ‘tourist hunting’ au professional hunting.

Abdulkadir alishauri serikali kuwa inapaswa kusikiliza na kutoa kipaumbele katika kuliangalia suala hili la ongezeko la kodi kwa jicho la tatu, kwa kuwa wasidhani kuwa watalii wanakuja Tanzania pekee.

 

Anasema Tanzania inashindana na nchi nyingi katika utalii hivyo ili kuendeleza sekta hiyo ni vyema serikali ikaondoa kodi ya VAT kwenye sekta ya utalii.

Kwa mtazamo mwingine Rais wa Tanzania John Magufuli amekataa kata kata kufuta kodi hiyo na kusema ni bora kuwa na watalii wachache wanaolipa kodi na kuchangia pato la taifa badala ya kuwa na utitiri wa watalii ambao hawalipi kodi. Alifafanua kuwa taarifa alizonazo zinaonesha watalii wengi wanaongezeka na hivyo kufuta jakamoyo hiyo.

Kiutalii Tanzania hupendelea watalii wenye pesa badala ya kapuku ambao huja na mikoba mgongoni na hawanunui vitu. Hivi basi imekuwa ikipata watalii wachache lakini matumizi yao yanali8ngana na wengi wa Kenya.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles