
Na Editha Karlo, BUKOBA
UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), umekilalamikia kitendo cha viongozi wa Chama cha Demokrasia Maendeleo (Chadema) kulitumia janga la tetemeko la ardhi kufanya propaganda za siasa.
UVCCM umeitaka na kuishauri Serikali iwaachie kazi ya uhakiki, ugawaji wa misaada yote kwa waathirika askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) .
Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Shaka Hamdu Shaka alikuwa akizungumza jana baada ya kukabidhi msaada kwa Mkoa wa Mkoa wa Kagera, Meja Jenerali mstaafu Salum Kijuu.
Alisema kinachofanywa na Chadema ni kituko na fedheha ya siasa kuona viongozi wake wakilitumia tetemeko hilo kujaribu kujijenga katika siasa huku kikiwabagua wanachana wa CCM jambo ambalo ni kinyume na ubinadamu.
Alisema uhakiki na utoaji wa msaada katika awamu ya kwanza ulifanyika kwa kuongozwa na vitendo vya ubaguzi na upendeleo huku baadhi ya shehena za mizigo ya misaada na vifaa vya ujenzi ikiandikwa maneno ‘Ukawa pamoja’.
“Kumefanyika ubaguzi na siasa potofu zikiongozwa na viongozi wa Chadema, tunaishauri Serikali kuwakwepa matapeli wa siasa na ubabaishaji. Hii kazi ya uhakiki, uratibu na ugawaji wa misaada waachiwe JWTZ ,” alisema Shaka.
Alisema katika uhakiki wapo watu wanaomiliki nyumba zaidi ya moja lakini majina yao yanapoonekana zaidi ya mara moja wamekuwa wakisumbuliwa bila sababu .
“Mkuu ipo haja tujue kuwa kuna wamiliki wa nyumba na wapangaji wote hawa katika janga hili ni waathirika wa tetemeko , mmoja ikiwa amepoteza nyumba, wengine wamepoteza ndugu, mali na vifaa vyao muhimu vya kuendeshea maisha,” alisema.