31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Utekaji, mauaji vyatikisa Kyela

Na Mwandishi Wetu, Kyela

WIMBI la utekaji na mauaji ya watoto wa kike katika Kata ya Itunge Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya linatisha.

Hali imezidi kuwa mbaya, baada ya watoto wa kike kutekwa na kuuawa kinyama, kisha kunyofolewa viungo katika sehemu za miili yao.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Itunge Kaskazini, Amasha Amasha alisema  siku tatu zilizopita kumekuwa na matukio ya utekeji wa watoto, jambo ambalo limezua hofu kubwa katika eneo hilo.

Alisema mwanafunzi wa kike anayesoma darasa la awali Shule ya Msingi Itunge (jina tunalo), alipotea lakini siku ya pili alikutwa amefariki dunia, huku akiwa amenyofolewa masikio, macho, ulimi na sehemu za siri.

Alisema siku iliyofuata, mtoto mwingine anayesoma darasa la sita katika Shule ya Msingi Itunge (13) alitekwa na watu waliokuwa wameficha sura zao.

Alisema baada ya kutekwa, mtoto huyo alipelekwa kwenye machimbo ya mchanga yaliyopo Kata ya Itope, lakini  wahusika wakiwa wameficha nyuso walimkataa na kudai wanahitaji mtoto wa kike.

Alisema tukio la tatu, lilitokea juzi baada ya mwanafunzi wa kidato cha pili shule ya Sekondari ya Itunge, Oliver Mwambije (18) kutekwa na watu wasiojulikana.

Alisema pamoja na juhudi za kumsaka mpaka jana, alikuwa hajaonekana. Alisema kutokana na hali hiyo, waliamua kupeleka taarifa kituo cha polisi kwa maandamano ili wasaidiwe.

Mwenyekiti wa Kitongoji cha Itunge Kati, Ibrahim Mwakanyamale alisema baada ya matukio hayo waliitisha mkutano mkuu wa vitongoji vyote kwa kuwashirikisha machifu wa kata za Mwaya, Ikolo na Kyela Mjini, lakini katika kikao hicho hawakufikia mwafaka.

Jeshi la Polisi mkoani Mbeya, limekiri kuwapo na tukio hilo ambao wanaendelea na uchunguzi wa kuwabaini wahusika wa mauaji hayo ili kuwafikisha mikononi mwa sheria.

Katibu Tawala Wilaya ya Kyela, Godfrey Kawacha, alikiri kuwapo  tukio hilo na kusema uchunguzi unaendelea.

Kuhusu mtoto aliyeuawa, Kawacha alisema mwili unaonekana kuchomwa na kitu chenye ncha kali.

Kuhusu mwanafunzi wa kidato cha pili aliyepotea katika mazingira ya kutatanisha, alisema kazi ya kumtafuta inaendelea.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi, alipoulizwa kuhusu matukio hayo alikiri kutokea na kusema wameanza msako.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles