27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

UNAJUA KILICHOPO KWENYE NDOA? – 2

JE, unatarajia nini kwenye ndoa yako ijayo? Unahitaji mafanikio au kuvurunda kila siku kwenye biashara zako? Kama unataka kuwa bora lazima uwe na mwenzi sahihi. Bahati mbaya rafiki zangu wengi wanajiandaa kwa mazuri tu kwenye ndoa zao na kusahau changamoto.

Hawana mpango na changamoto na migogoro, hapo watakuwa wanakosea sana. Kama mnakumbuka vizuri, wiki iliyopita nilifafanua juu ya baadhi ya watu kuishi  maisha ya kuigiza.

Kutoigiza hutampa nafasi mpenzi wako kuishi maisha yake ya kawaida, mwisho kila mmoja atamjua mwenzake.  Tuendelee na somo letu…

KEMEA MAPEMA MATATIZO
Katika kuishi kwako maisha yako halisi, mwenzako naye atakuwa kama wewe. Hiyo ni hatua nzuri maana itakuwa rahisi sana kwako kugundua tabia za mwenzako. Hapo utazijua nzuri na mbaya.

Acha kulea matatizo, bila kujali jinsi, mwambie mpenzi wako tabia ambazo hazikufurahishi. Ili aweze kubadilika kwa urahisi zaidi, unatakiwa kumwambia kwa utaratibu, lakini pia umpe sababu za wewe kukataa tabia zake hizo.

Akiendelea nazo kuwa mkali, wakati mwingine ukali unasaidia. Kwa kukemea kama ni kweli anakupenda na anahitaji uhusiano wenu uendelee, basi lazima atabadilika.

Akifanya hivyo itakuwa vizuri zaidi kwako, maana utakuwa na uhakika angalau kwa asilimia chache kwamba mpenzi wako anakusikiliza.

TABIA ZA ASILI
Rafiki zangu, lazima ufahamu kwamba wakati unapambana na tabia za mpenzi wako zisizokupendeza, zipo tabia nyingine ni za asili. Hazibadiliki. Sasa hapo lazima uwe makini kwa mambo mawili; Mosi, zitakuathiri?

Pili, ni tabia zitakazokugombanisha na jamii? Maana kuna tabia nyingine zinavumilika, lakini je, hazitaleta athari kwa majirani zenu watarajiwa? Haya ni mambo ya kuyatafakari kabla ya kuingia kwenye ndoa.

Mathalani, kuna baadhi ya watu wana viburi au dharau za kuzaliwa! Hata umfanyeje, habadiliki. Unaweza kumwuliza kitu akanyamaza.

Ni tabia ya kiburi, lakini kwa sababu amezaliwa akiwa na tabia hiyo, hawezi kuiacha. Sasa hapo lazima ujiulize, utawezana naye?

Utaweza kumvumilia na kiburi chake kwa maisha yenu yote? Huu ni mfano tu rafiki zangu, zipo tabia nyingi za asili, ambazo kwa nafasi yako unaweza kuzichunguza kwa mpenzi wako kabla ya kuchukua uamuzi mzito wa kuingia kwenye ndoa. 

KUWA MKWELI
Ukweli ni silaha, ni haki na siku zote humfanya mtu awe huru. Kama kuna jambo ambalo hujalipenda kwa mpenzi wako, haraka mwambie. Acha kukaa na vitu moyoni. Si utaratibu mzuri.

Hata kama nguo zake hazikufurahishi mwambie: “Baby yaani kiukweli ukivaa hizo jeans zako hupendezi kabisa. Nadhani uanze kuvaa suruali za vitambaa.”

Hapo utakuwa umemwambia ukweli wako, kukubaliana na wewe au kukataa kutatokana na mapenzi yenu wewe na yeye. Kama anakupenda atakusikiliza. Kwani anamfurahisha nani huko barabarani zaidi yako? Kuwa mkweli.

UTARATIBU WA KAZI
Suala la kazi kwa baadhi ya wanandoa huwa ni tatizo. Utakuta mwanaume amemkuta binti wa watu anafanya kazi, wamependana na kufunga ndoa. Ghafla anamwambia mwenzake aache kazi!

Ndoa nyingi hasa changa huingia kwenye mgogoro huu. Kwangu mimi wanandoa wote kufanya kazi ni bora zaidi, maana ile maana ya usaidizi wa mwanamke inakuwa imekamilika.

Kwa maisha ya sasa mama kukaa nyumbani siyo ‘dili’ tena. Hata hivyo ili kuepusha matatizo, suala hili ni vyema mkajadiliana mapema. Kaa na mwenzako, mwulize: “Lakini darling, vipi kuhusu kazi baada ya kufunga ndoa?”

Anzisha huu mjadala na mwisho muwe na majibu yenye usawa. Mkubaliane kwa pamoja. Vijana wa kileo  wanasema, ‘kwa roho safi’. Hii itakusaidia maana mgogoro huu utakuwa umeisha kabla hata ya ndoa yenu.

Usikose sehemu ya mwisho ya mada hii wiki ijayo.

Jiandae kupokea kitabu changu kipya cha SIRI ZA NDOA YENYE FURAHA kitakachokuwa mitaani hivi karibuni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles